Kayihura aweka wanasheria kumtetea

Muktasari:

Jenerali Kayihura alikamatwa wiki iliyopita kutoka shambani kwake Kashagama, wilayani Lyantonde na akasafirishwa hadi Kampala na kwa sasa anahojiwa kuhusu masuala kadhaa katika katika kambi ya Makindye.

Kampala, Uganda. Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) wa zamani aliyewekwa katika kizuizi cha kambi ya jeshi ya Makindye Jenerali Kale Kayihura amekataa kutoa ushirikiano kwa maofisa wa jeshi na polisi wanaomhoji.
Badala yake mkuu huyo wa zamani wa Jeshi la Polisi ameajiri wanasheria wawili kwa ajili ya kushughulikia suala lake na ametaka afikishwe kwenye mahakama ya kiraia.
Jenerali Kayihura alikamatwa wiki iliyopita kutoka shambani kwake Kashagama, wilayani Lyantonde na akasafirishwa hadi Kampala na kwa sasa anahojiwa kuhusu masuala kadhaa katika kambi ya Makindye.
Hata hivyo, vyanzo vilivyo karibu na idara ya upelelezi vinasema kwamba amekataa kutoa ushirikiano kwa timu ya wapelelezi, ambao anawatuhumu kwamba wanamuonea.
Jopo la wapelelezi wanaomhoji inadaiwa linajumuisha Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi (CDF), Jenerali David Muhoozi, Waziri wa Usalama Jenerali Elly Tumwine, Kamanda wa Upelelezi Jeshini (CMI) Brigedia Abel Kandiho, Mkurugenzi wa Shirika la Upelelezi wa Ndani (ISO), Frank Kaka Bagyenda, Mkurugenzi wa Kupambana na Ugaidi Abbas Byakagaba pamoja na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Grace Akullo.
Vyanzo hivyo vinasema kwa siku mbili, alikuwa akishirikiana vizuri na timu ya upelelezi lakini walipoanza kumhoji maswali yanayomhusisha na kifo cha aliyekuwa msemaji wa polisi Andrew Kaweesi na ujasusi, inaelezwa alibadilika na akakataa kutoa ushirikiano akitaka akutane na wanasheria wake.
Alipofuatwa ili afafanue madai hayo, msemaji wa polisi Brigedia Richard Karemire alikataa kutoa maelezo ya kina, akiishia kusema Jenerali Kayihura ana haki ya kuonana na wanasheria wake na kwamba taarifa nyingine yoyote itakuwa inatolewa kwa utaratabu pale inapobidi.