Mazishi kitaifa ya Bush kesho

Muktasari:

  • Jumatatu usiku Rais Trump na mkewe Melania Trump walitoa heshima zao za mwisho kwa hayati Bush katika ukumbi wa makao makuu ya Serikali Capitol Rotunda.

Washington, Marekani. Rais Donald Trump anatarajiwa kuwaongoza maelfu ya wananchi, wakiwamo waliokuwa marais wa nchi hiyo katika mazishi ya kitaifa ya hayati George H. W. Bush yatakayofanyika kesho.
Marais wa zamani wanaotarajiwa kuhudhuria ni Barack Obama, George W. Bush, Bill Clinton na Jimmy Carter pamoja na wake zao. Viongozi hao pamoja na waombolezaji wengine pia wanatarajiwa kuhudhuria misa ya kumwombea Bush itakayofanyika katika Kanisa Kuu la Dayosisi jijini Washington.
Jumatatu usiku Rais Trump na mkewe Melania Trump walitoa heshima zao za mwisho kwa hayati Bush katika ukumbi wa makao makuu ya Serikali Capitol Rotunda. Mwili wake kwa sasa umewekwa Capitol Hii. Trump na mkewe walitumia sekunde 15 kutoa heshima za mwisho.
Wabunge wa mabaraza yote – baraza la wawakilishi na seneti pia walitoa heshima zao kwa Rais huyo wa zamani aliyefariki dunia wiki iliyopita.
 Msemaji wa baraza la wawakilishi, Paul Ryan alimsifu marehemu na kumtaja kuwa mzalendo mashuhuri kabisa.
Makamu wa Rais wa Marekani, Mike Pence pia aliaga mwili wa Rais huyo wa 41 aliyeitawala Marekani muhula mmoja kuanzia mwaka 1989 hadi 1993. Chini ya utawala wake, Marekani ilifanikiwa kumaliza vita baridi.
Mbwa wake
Mbwa wa hayati Bush ambaye amekuwa akimhudumia mkuu huyo wa zamani enzi za uhai wake alikuwa akionekana amelala kando ya jeneza na alisafirishwa ishara ya kusindikiza maiti kutoka Houston, Texas hadi Washington, DC. Mbwa huyo anaitwa Sully H.W. Bush