Messi, baba yake jela miezi 21

Mshambuliaji wa Argentina na Barcelona, Lionel Messi na Baba yake, Jorge Messi wamehukumiwa kifungo cha miezi 21 jela. Picha ya Getty Images

Muktasari:

  • Baba yake, Jorge Messi, pia amehukumiwa kifungo kwa kukwepa kulipa kodi inayokadiriwa kufikia Euro 4.1 milioni kwa kipindi cha kuanzia 2007 hadi 2009.

Barcelona, Hispania
Mshambuliaji wa Argentina na Barcelona, Lionel Messi amehukumiwa kifungo cha miezi 21 jela kutokana na kukwepa kulipa  kodi, vyombo vya habari vya Hispania vimeripoti.

Baba yake, Jorge Messi, pia amehukumiwa kifungo kwa kukwepa kulipa kodi inayokadiriwa kufikia Euro 4.1 milioni kwa kipindi cha kuanzia 2007 hadi 2009.
Pia, wawili hao watakumbanana na faini ya mamilioni ya Euro kwa kutumia njia za ulipaji wa kodi wa Belize na Uruguay, ambako kuna kiwango cha chini, zilizokuwa na lengo la kujipatia kipato cha haki za picha zake (Messi).
Hata hivyo, Messi mwenye tuzo tano za mchezaji bora wa dunia wa Fifa na baba yake wanaweza kukwepa maisha ya jela.
Kwa mujibu wa sheria za Hispania, kipengele cha kwenda jela chini ya miaka miwili kinaweza kutumikiwa kwa makubaliano maalumu.
Mshambuliaji huyo wa Barca na baba yake walikutwa na hatia ya makosa matatu katika kodi wakati wa hukumu ya jana katika Mahakama ya Barcelona.
Wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo, Lionel Messi alisema kwamba 'hajui chochote' juu ya usimamizi wa fedha zake, akidai kuwa kazi yake ni 'kucheza mpira'.