Polisi waanika mali walizokamata kwa waziri mkuu

Muktasari:

  • Tangu alipoangushwa na Mahathir Mohamad katika uchaguzi mkuu wa Mei mwaka huu Najib amezuiwa kuondoka nchini na amekuwa akihojiwa na tume ya kupambana na ufisadi hadi kufikia nyumba zake na za familia kupekuliwa.

Kuala Lumpur, Malaysia. Polisi wametangaza kuwa wamekamata mabegi ya fedha taslimu, vito vya thamani, pochi, saa na vitu vingine kutoka maeneo yenye uhusiano na aliyekuwa waziri mkuu Najib Razak vyote vikifikia thamani ya dola za Marekani 273 sawa na Sh.621.5 bilioni.
Mkuu wa polisi kitengo cha uhalifu wa kibiashara nchini Amar Singh, Jumatano aliwaambia wanahabari kwamba gharama ya vitu vyote vilivyokamatwa kutoka majumba sita ambayo yanahusishwa na Najib ni kati ya dola 224 milioni na dola 273 milioni.
"Hatukuweza kukokotoa thamani yake kwenye maeneo husika kwa sababu viwango vilikuwa vikubwa sana," alisema Singh na kuongeza kuwa mali iliyokamatwa ndiyo kubwa zaidi katika historia ya Malaysia.
Mkuu huyo wa polisi alisema iliwachukua muda wa siku tatu tena kwa msaada wa mashine sita ya kuhesabia na maofisa 22 kutoka Benki Kuu ya Malaysia kuhesabu fedha zilizokamatwa katika maeneo hayo, na akaongeza kiasi cha dola 28.9 milioni kilikamatwa kikiwa katika aina 26 tofauti ya fedha ikiwemo ringgit ya Malaysia.
Mamlaka zinamchunguza Najib ikiwa ni sehemu ya uchunguzi wa fedha zilizopotea kifisadi katika mfuko wa maendeleo ya miradi uitwao 1MDB uliokuwa umeasisiwa na waziri mkuu huyo.
Tangu alipoangushwa na Mahathir Mohamad katika uchaguzi mkuu wa Mei mwaka huu, Najib amezuiwa kuondoka nchini na amekuwa akihojiwa na tume ya kupambana na ufisadi hadi kufikia nyumba zake na za familia kupekuliwa.