Rais Buhari ateua waliokufa

Dar es Salaam. Uteuzi wa wajumbe wa bodi za taasisi za Serikali uliofanywa na Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria umeibua utata baada ya baadhi ya majina kubainika kuwa ni ya watu waliofariki dunia.

Orodha ya watu 1,460 ilitolewa Ijumaa jioni, lakini ilipochambuliwa kwa makini ilionekana kuna majina ya watu waliofariki muda mrefu na baadhi ambao hawako chama tawala.

Hata hivyo, akiongea na vyombo vya habari, msemaji wa rais amepuuza taarifa hizo akisema ni za kukuza mambo.

Miongoni mwa majina ambayo yamebainika kuwa ni ya watu waliokufa ni jina la seneta wa zamani, Francis Okpozo. JIna hilo lilifanya vyombo vya habari vipekue zaidi kwenye orodha hiyo na kukuta majina mengine ya waliokufa, akiwemo Garba Attahiru na Umar Dange.

Femi Fani-Kayode, waziri wa zamani, alisema kugundulika kwa majina hayo kunaonyesha kuwa Rais Buhari ana matatizo ya afya ya akili. Gazeti la The Post limemkariri Fani-Kayode akimuhusisha rais huyo na imani za kichawi, akisema anaziabudu na kuzikuza.