Trump adai Urusi haikuingilia uchaguzi wa Marekani 2016

Muktasari:

  • Rais wa Marekani, Donald Trump ameitetea Russia na tuhuma kwamba iliingilia uchaguzi wa rais nchini mwake mwaka 2016.

Vigogo wa Congress wadai ameitia aibu Marekani, vyombo vya habari vyamshukia

Helsinki, Finland. Rais wa Marekani, Donald Trump ameitetea Russia na tuhuma kwamba iliingilia uchaguzi wa rais nchini mwake mwaka 2016.

Baada ya mazungumzo ya ana kwa ana na Rais wa Russia, Vladmir Putin yaliyodumu kwa saa mbili, Rais Trump aliyapinga mashirika ya ujasusi ya Marekani akisema hakukuwa na sababu yoyote ya Russia kuingilia uchaguzi wa Marekani.

Kwa upande wake, Rais Putin alisisitiza kwamba kamwe nchi yake haijawahi kuingilia uhusiano wake na Marekani kwa nia ya kuuharibu.

Kabla ya mkutano huo, viongozi wa Demokratic walimuonya Trump wakimtaka awe mwangalifu dhidi ya Putin huku wengine wakisema kuwa haukuwa uamuzi mzuri kwa rais wa Marekani kufanya mkutano wa aina hiyo.

Trump alitakiwa na mwandishi kueleza baada ya kuandika mapema kwenye mtandao wa Twitter kuwa Marekani inalaumiwa kwa hali tete ya sasa kati yake na Russia.

Alisema pande zote zilifanya makosa lakini akakataa kugusia mambo kadhaa yakiwemo kuhusika kwa jeshi la Russia nchini Ukraine na kulimega eneo la Crimea, shambulizi la kutumia kemikali ya novichok kusini mwa England na kushtakiwa kwa raia wa Russia kwa kuingilia kati uchaguzi wa Marekani.

Badala yake, alisisitiza kuwa hakukuwa na ushirikiano kwa njia yoyote ile kati ya timu yake ya kampeni na Russia.

Alipoulizwa ikiwa anaweza kuishutumu Russia na Putin moja kwa moja kwa kuingilia kati uchaguzi, Trump alisema maofisa wake wa ujasusi, akiwemo mkurugenzi Dan Coats walimwambia kuwa wanafikiri kuwa ni Russia, lakini baadaye Putin alimwambia nchi yake haikuhusika.

Viongozi wamjia juu

Kiongozi wa wachache katika Bunge la Senate, Chuck Schumer aliitaja hatua ya Trump kuwa ya aibu ambayo ilikuwa hatari na dhaifu.

John Brennam, mkurugenzi wa CIA wakati wa uongozi wa Barack Obama alisema Trump alifanya makosa ya ‘uhaini’.

Mgombea urais kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2008 nchini Marekani, John McCain alisema alichofanya Trump ni kitendo kibaya zaidi na hakijawahi kufanywa na rais wa Marekani.

Baada ya kukutana katika mkutano wake wa kilele na mwenzake wa Russia nchini Finnland, Trump alisema dunia inatamani kuona uhusiano mwema baina ya mataifa hayo. Mkutano huo uliofanyika mchana ulikuwa ukifuatiliwa kwa karibu na viongozi wa dunia na hasa barani Ulaya.

Trump alifungua mkutano huo kwa kusema kwamba ulimwengu unataka kuiona Russia na Marekani zikiwa katika uhusiano mzuri.

Upande wake, Putin alisema amekuwa akiwasiliana kwa simu na Trump pamoja na kukutana katika matukio ya kimataifa, lakini umewadia wakati wa kuwa na majadiliano ya kina kuhusu matatizo mbalimbali ya kimataifa.

Spika wa Bunge la Congress nchini Marekani, Paul Ryan alisema katika taarifa yake kuwa Russia iliingilia uchaguzi na inaendelea kujaribu kuikandamiza demokrasia nchini Marekani na duniani kote.

Alisisitiza kuwa Marekani lazima ijikite katika kuiwajibisha Russia na kumaliza mashambulizi yake mabaya ya demokrasia.

Kiongozi wa wachache wa Congress, Nancy Pelosi alisema udhaifu wa Trump mbele ya Putin ulikuwa wa kutia aibu.

Pia kiongozi huyo wa Democratic alisema tabia ya Trump inadhihirisha kuwa Russia wana kitu fulani dhidi ya kiongozi huyo cha binafsi, kifedha au kisiasa.

Vyombo vya habari

Shirika la Habari la ABC lilisema Trump alikubali madai ya Putin kuwa Taifa la Russia halijawahi kuingilia uchaguzi wa Marekani na alikataa fursa ya kuliwajibisha kwa makosa ambayo yalifanyika katika nchi ambayo anaiongoza.

Gazeti la Washington Post liliandika kuwa Rais Trump hawezi kupinga upingaji wa Putin, lakini amemkaribisha vizuri rais huyo wa Russia na kuendelea kulalamikia uchunguzi wa mamlaka za kiitenligensia za Marekani.

Uchaguzi wa Rais wa Marekani, mwaka wa 2016 ulikuwa wa 58 katika historia ya nchi hiyo. Ulifanyika Novemba 8, 2016.

Katika uchaguzi huo, Trump aliyepeperusha bendera ya Republican pamoja na makamu wake, Mike Pence alimshinda mgombea wa Democratic, Hillary Clinton aliyekuwa na mgombea mwenza, Tim Kaine.