Kingunge ashangazwa na uvumi kuhusu hali yake

Muktasari:

Kingunge amesema leo asubuhi amefanya mazoezi ya kutembea kwa saa moja na nusu.

Dar es Salaam. Mwanasiasa mkongwe nchini Tanzania, Kingunge Ngombale Mwiru amewashangaa wanaoeneza taarifa kuwa yu mgonjwa na amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Akizungumza na Mwananchi leo Ijumaa Novemba 10,2017 nyumbani kwake Makumbusho jijini Dar es Salaam amesema yuko vizuri na hana tatizo lolote.

Amesema anaendelea kudunda kama kawaida na kwamba leo asubuhi alifanya mazoezi ya kutembea kwa saa moja na nusu ili kuuweka sawa mwili wake.

Kingunge ameshauri kupuuzwa taarifa za mitandao zinazosambazwa kueleza kuwa yu mgonjwa.

Tangu jana Alhamisi Novemba 9,2017 kwenye mitandao ya kijamii imesambazwa picha ikimuonyesha Kingunge akiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili akijuliwa hali na Rais mstaafu Jakaya Kikwete na mkewe Salma.

Kingunge aliyekuwa kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM), alijiondoa katika chama hicho Oktoba 4,2015  kabla ya Uchaguzi Mkuu na alisema hatajiunga na chama chochote.