Kingunge arejeshwa Muhimbili

Dar es Salaam. Mwanasiasa mkongwe nchini, Kingunge Ngombare Mwiru amerejeshwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ili kuendelea na matibabu.

Kingunge aliruhusiwa kutoka hospitalini hapo Januri 10, 2018 ili kwenda kushiriki tukio la mazishi ya mkewe ,Peras Ngombare Mwiru yaliyofanyika jana katika makaburi ya Kinondonbi jijini Dar es Salaam.

Pares aliyefariki dunia Januari 4, katika hospitali ya Muhimbili alikokuwa amelazwa kwa ugonjwa wa kupooza huku Kingunge naye akilazwa hospitalini hapo akiuguza majeraha ya kushambuliwa na mbwa nyumbani kwake, Victoria jijini humo hivi karibuni.

Akizungumza na Mwananchi leo Januari 12, 2018, mtoto wake, Kinje Ngombare Mwiru amesema baada ya baba yake kupata kumzika mkewe amerejea hospitalini ili kuendelea na matibabu kama alivyotakiwa na madaktari wake.

“Leo Mzee (Kingunge)  amerudishwa hospitalini tayari kwa ajili ya kuendelea na matibabu na amelazwa ICU (chumba cha wagonjwa mahututi) cha Mwaisela na hali yake inaendelea vizuri,” amesema Kinje.