Kisa cha Lipumba kutaka kubaki CUF

Mwenyekiti wa CUF,Profesa Ibrahimu Lipumba

Muktasari:

Wako wanaomuelewa na kumuunga mkono, wakiongozwa na Magdalena Sakaya, mbunge wa Jimbo la Kaliua, moja ya majimbo ya mkoani Tabora ambako Lipumba alikuwa akitajwa kuwa angegombea ubunge mwaka jana.

Dar es Salaam. Wakati Profesa Ibrahim Lipumba anatangaza kujivua uenyekiti wa CUF, nchi ilizizima; maswali, tuhuma za usaliti na ubashiri yakatawala akili na mazungumzo mitaani.

Lakini, ukimya uliofuatia baada ya kwenda nje ya nchi kwa kile kilichoelezwa kuwa ni mapumziko, kuliondoa tuhuma hizo na maswali.

Sasa uamuzi wake wa kutengua barua yake ya kujiuzulu na jitihada zake za kurejea kwenye kiti chake CUF, zimerejesha tena maswali, tuhuma za usaliti na ubashiri wa hatima yake.

Wako wanaomuelewa na kumuunga mkono, wakiongozwa na Magdalena Sakaya, mbunge wa Jimbo la Kaliua, moja ya majimbo ya mkoani Tabora ambako Lipumba alikuwa akitajwa kuwa angegombea ubunge mwaka jana.

Lakini, CUF inamuona kama msaliti anayetaka kuvuruga chama baada ya kukiacha wakati kikiwa kwenye kipindi kigumu cha uchaguzi mkuu mwaka jana.

Chadema inamuona Lipumba kuwa ni mtu anayetaka kuvunja Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kutokana na msimamo wake dhidi ya Edward Lowassa, aliyepewa fursa ya kugombea urais kwa tiketi ya Chadema na kuungwa mkono na CUF, NLD, NCCR-Mageuzi na ambavyo pamoja na chama hicho kikuu cha upinzani vinaunda umoja huo.

Lipumba pia anaungwa mkono na kikundi cha wafuasi na wanachama wa CUF cha jijini Dar es Salaam ambacho kilivunja mlango wa ofisi za chama hicho kumuwezesha kuingia baada ya Msajili wa Vyama vya Siasa kutoa msimamo wake kuhusu hali ya uongozi, akimtambua profesa huyo kuwa mwenyekiti halali.

Hali hiyo iliifanya Mwananchi kuandaa maswali manne kwa ajili ya kuhoji wachambuzi kuhusu uamuzi wa Lipumba kubadilisha msimamo wake wa kujivua uongozi na kuweka msisitizo kuwa ndiye mwenyekiti halali wa CUF.

Moja ya maswali hayo ni sababu zilizomfanya Profesa Lipumba atake kurejea CUF sasa-zaidi ya mwaka mmoja baada ya kujitoa? Je, ana nia ya dhati kukijenga chama kwa mtazamo anaouona sahihi? Kutokuwa na kazi nje ya siasa? Au ni upepo wa kisiasa wa sasa?