DC Hai atoa siku 45 gereji kuhamishwa

Muktasari:

Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya ameagiza  kuondolewa gereji zote zilizojengwa pembezoni mwa barabara katika mji wa Bomang'ombe. Wahusika wamepewa siku 45 kuondoka eneo hilo.


Hai. Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya ametoa  siku 45 kwa wananchi waliovamia hifadhi ya barabara katikati ya mji wa Bomang’ombe na kujenga gereji kuondoka katika maeneo hayo.

Ametoa agizo hilo leo Desemba 7, 2018 katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Snow View wilayani Hai wakati akisikiliza kero za wananchi.

Amesema gereji hizo zimejengwa kinyume na taratibu hali inayochangia mji huo kuonekana mchafu, mpangilio mbovu.

“Nimeelekeza kuanzia sasa gereji zaidi ya 6 ambazo zipo pembezoni mwa barabara ziondolewe kwa kuwa zimejengwa kinyume na taratibu. Nimewapa siku 45 waondoke ili kuupa heshima mji wenu na kuupanga ukae vyema,” amesema Sabaya

 

 

 

“Hatupingi mtu kujitafutia riziki lakini tunataka mji wetu uwe katika utaratibu na mpangilio mzuri. Nimemuagiza mkurugenzi kuwapatia maeneo mengine ya kuweka gereji zenu ili muendelee kuchapa kazi.”

 

Naye  mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo, Yohana Sintoo amesema wametenga  eneo la ekari moja lililopo umbali wa mita 100 kutoka barabarani kwa ajili ya kuzihamishia gereji   hizo.

 

John Joel,  mmoja wa mafundi gereji amesema kitendo cha kuondolewa katika maeneo waliyoyazoea ni ngumu kwa uwa wanahofia kupoteza wateja.

 

“Hatuwezi kukataa kuondoka kwa sababu wenye mji wao wameamua, tunachoomba ni kupatiwa eneo jingine ambalo litatutosha kwa ajili ya kuendelea na shughuli yetu,” amesema.