Kampuni ya Tata yaingiza sokoni gari zake za kisasa

Muktasari:

Kampuni ya Tata Motors imetangaza kuanza kuuza magari yake aina ya Tata NEXON na Tata HEXA katika bara la Afrika na mnunuaji ataweza kulipa kidogokidogo kwa mwezi.

Dar es Salaam. Gari aina ya Tata NEXON na Tata HEXA zilizozinduliwa India mwaka 2017, zimetangazwa rasmi katika soko la Afrika huku mnunuzi akipewa chaguo la kuamua kulipa kidogokidogo kila mwezi.

Kampuni ya Tata Motors jana Jumamosi Novemba 2,2018 ilitangaza kuanzia siku hiyo magari hayo yatakuwa yakipatikana nchini Tanzania na Afrika kwa ujumla kupitia kwa mawakala wao walioidhinishwa.

“Tunafurahi kutangaza uzinduzi wa gari zetu hapa nchini. Gari zote zimetengenezwa katika ubunifu wa kisasa, viwango bora na teknolojia endelevu. Kwa uzinduzi huu tunatarajia kuongeza ukubwa wetu katika soko hapa nchini,” amesema Mkuu wa biashara za kimataifa wa Tata Motors, Sujan Roy.

Amesema ana imani bidhaa hiyo imeingia sokoni wakati mwafaka na wanunuaji wote watapata ofa ya bima isiyozidi Sh2.5 milioni sanjari na waranti ya miaka 3 kwa Kilimeta 60,000 tu.

Kadhalika amesema uuzwaji wa gari hizo umewekewa urahisi kwani mtu ataweza kulipa kwa kila mwezi “Tunafikiria kujenga kiwanda cha kuunganishia magari hapa kwa baadaye ili kuendelea kuweka unafuu zaidi wa bei ya magari yetu”.

Mkuu wa Tata Holdings Limited kanda ya Afrika Mashariki, Naresh Leekha amesema: “Hii ni hatua ya kwanza kubwa kufikiwa . Tunajivunia na tuna imani kuwa tutafanya hivi tena katika bidhaa nyingine bora kwa siku zijazo.”