Kero ya Fiesta na utani wa wanaume wa Dar...

Kulia alikaa Minner, mwenye macho makubwa, na ngozi laini mno. Ukitaka kumpapasa uwe muangalifu. La sivyo kesi ya kutoboa mwili itakuhusu. Katikati alikaa Dora, mwenye mwanya, maji ya kunde. Nywele zake fupi ziking’aa kwa futa. Mtazame Flaviana Matata uipate picha yake kamili.

Kushoto alikuwepo Nana Cute. Mchanganyiko wa Kimbulu na Kibondei. Lafudhi ya Tanga, rangi ya Kiarusha. Alivutia akicheka. Alivutia kwa umbo lake. Majina yao siyo halisi niliyafahamia kwenye ‘grupu’ la whatsApp. Mpaka dakika hiyo sikuyajua majina halisi. Pia sikuhitaji kuyajua.

Walikuwa ‘bize’ kuchati, mianga ya simu ilinipa nafasi ya kuona ufundi wa Mungu katika kuumba sura za viumbe uzao wa Eva. Sikutaka ushahidi zaidi kujua kama wanafaa. Siyo tu kwa ngono za usiku mmoja, bali kwa maisha yote milele amina. Tabia kitu gani bana? Tutaelekezana ndani ya nyumba.

Niliwatazama kupitia kioo cha ndani ya gari. Ni warembo kwa maana ya urembo. Na siyo tu zaidi ya urembo. Pia mimi sikufaa kuwamiliki hata mmojawapo. Nikameza mate nikikaza mishipa ya shingo kama kamba za viatu. Huku nikitegemea upeo na uongo zaidi ya muonekano na kipato changu.

Niliwaangalia kwa jicho la ufundi. Sikuona kasoro yao. Nasema hivi kwa sababu nilikuwa na akili zangu timamu. Kama ingekuwa amri yangu ningeenda mbele zaidi kwa kuwaposa na ikibidi kufunga nao pingu za maisha kwa pamoja.

Nielewe ninaposema warembo. Kama ubora wao ulinifanya niwaone malaika nikiwa macho makavu, ningekuwa nimelewa huenda ningewaona kama Miungu ya kike. Miaka yote ya kuishi duniani, nawajua wasichana wazuri. Hawa walikuwa wazuri kuliko uzuri wenyewe. Mawazo yalikatishwa na sauti ya mmoja wao aliyeuliza hapa ni wapi? Tukipita maeneo ya Mlimani City. Lafudhi yake ya Kiarusha, ghafla akili ikajirudi na kukumbuka kuwa nipo na madem wa mkoani. Nipo nao ‘grupu’ moja na sasa walikuwa wapo Dar kwa ajili ya tamasha la Fiesta.

Mimi na mshikaji wangu Derick (dereva), tulikuwa wenyeji wao. Tumetoka kuwapokea Ubungo. Kila kitu kigeni kwao. Wakitaka kujua kila sehemu wanayoisikia kwenye vyombo vya habari na kwa marafiki. Swaga zao zikanikumbusha utani wa wanaume wa Dar.

Hivi wanaume wa Dar ni kina nani? Viongozi wakuu wa nchi wote wako Dar. Matajiri na mastaa kama wote pamoja na timu za soka zile kubwakubwa zote zipo Dar. Katika hao wengi wao asili na makuzi yao yameanzia mikoani. Lakini wanaunganishwa kama wanaume wa Dar.

Kwa nini wanaume wa Dar kiwe kielelezo cha mtu dhaifu? Legelege? Nyanya? Zuzu? Boya lenye ubwege ndani yake? Kwa hiyo kila nyanja nchi hii inawakilisha taifa kimataifa na wanaume mazuzu? Narenare wenye ulegevu legevu? Mnatania au? Samatta naye pia ni wa Dar msijisahau.

Wanaume wa mikoani kile wanachoamini kama ndo ukakamavu, kumbe ni ubwege. Maisha ya kuchoma visu wanawake na kuwatia makovu ndo uanaume?

Au kutojihusudu kwa pamba na fujo za cheni shingoni na mbwembwe flan amazing ndo uanaume?

Hii leo wakipewa nafasi wanaume kadhaa wa Dar wakaenda mikoani. Na wa mikoani wakaja Dar. Kwa usiku mmoja tu kesho yake waulizwe. Ndipo hapo utakapoelewa kuwa masela wa Dar wanyime chakula lakini wape kitoweo uzao wa Eva. Ndo maana ‘guest’ nyingi kuliko nyumba za ibada.

Dar mtu kalazwa miguu ina vyuma huku ameshikilia drip. Bado anawaza kummendea ‘muuguzi’. Ndio maana wadada wengi wa mikoani wanaokuja Dar kufanya kazi za ndani. Wanakuja na usichana wao wanarudi njia nyeupe pee.

Toka enzi za kina Mtemi Isike Mirambo na kina Mkwawa. Mmekariri kifo cha mende.

Haya yanasemwa na dada zenu wakija Dar. Ndo maana hawarudi huko mikoani wakitua Dar. Wanaamua kufanya kazi za baa. Kupamba video za wasanii na kudanga mjini.

Dar kuna staili kibao kama toroka uje, popo kanyea mbingu, mwana ukome, kidole koleo, sugua gaga, peperusha, kiokote, mbuzi kavunja miguu ya mbele, pangaboi, komba mwiko nk. Wanapewa ujanja na udambwi udambwi kibao mpaka wanasahau kurudi kwao. Wacha muelezwe ukweli maana tumevumilia sana maneno yenu. Pengine ni kutaka kupata ujiko kwa kututajataja kwa madem zenu. Sasa tutavamia mikoani tuwaachie kilio. Kilio chenyewe ni cha kulea watoto wasio wenu na wajomba wasio na baba.

Sifa ya wanaume wa Dar ni uvivu wa kulea. Wanajua kuzalisha matunzo huachia Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo atende muujiza. Lakini kuwafanya kama mfano wa viumbe legevu mnakosea. Ina maana mnashindwa ‘kushea’ maongezi na dada zenu waliopo Dar wawaeleze ukweli.

Amber Lulu ni miongoni mwa wasichana wa kike mjini. Ambao walipokuja Daslama mjini kwa mara ya kwanza wakakamata ‘laini’. Kupitia video vixen tu. Umemfuatilia Amber Lulu wa leo? Ni dem ambaye utamuhusudu kwa ‘intavyuu’ tu. Huyu ni mmoja wa mabalozi wa wanaume wa mikoani na Dar. Ndiyo, kwa kila hali hakuwa msichana wa kawaida. Macho yake hayakuficha chochote ambacho angependa kuficha bila mimi kumshuku. Hata hivyo, hilo halikudhibiti ule ‘unyama’ wangu katika kumiliki viumbe uzao wa Eva. Tabia haina dawa. Ni tabia ya ‘unyama’ iliyofanya nianze udadisi. Kuchunguza ubora wa msichana huyu.

Muda huu alikuwa akipaka mafuta mwilini. Hana aibu kwangu tena. Siyo Dora yule mgeni kutoka Arusha. Alishaanza kuniita baby. Hapa ndipo nilipogundua mengi ya urembo wa Dora. Niliyemuona kwenye gari mara ya kwanza jana yake. Ni tofauti na Dora huyu wa ndani. Mzuri mara saba zaidi.

Nilichoona mara ya kwanza ni takataka kama takataka zingine. Huyu aliyekuwa ndani mbele yangu ndiye Dora mwanamke mrembo wa dunia yangu. Shingo yake ndefu aliilaza upande kidogo, macho yake yakizidi kulainika huku vidole vikiitua glasi ya kinywaji chake mezani.

Ilikuwa picha ya kusisimua, kuvutia, iliyofanya fikra zangu zichukue likizo na nafasi kuchukuliwa na hisia za ajabu za kimaumbile zilizonifanya niwaze. Raha ya kukumbatiwa na mrembo. Hakuna burudani kama kukumbatiwa na mikono laini. Hakuna cheo bora na kikubwa kama ‘kumbusu mrembo’.

Mtoto alikuwa tayari kwa mechi. Beki ziliacha goli wazi tayari kuruhusu mashambulizi ya kutosha. Si mimi wala Dora aliyekumbuka tumewaacha wapi wenzetu. Derick, Minner na Nana Cute hatukujua wako wapi kwa muda huo. Wala hakuna aliyejali kati yetu.

Kwanini tulikuwa ndani? Ni baada ya kusitishwa onesho la Fiesta wiki iliyopita. Wageni wetu wakaamua tulewe na kuzunguka kila ukumbi mzuri wa muziki au baa maarufu. Tukalewa wote.

Mimi na Dora tukahamia eneo tengefu. Hasira za Fiesta na kejeli za wanaume wa Dar. Dora atakuwa shahidi namba moja kwa kaka zake.

Kufidia hasira za kukosa onyesho la Fiesta. Tukaamua tuwatembeze wageni wetu maeneo yote waliyotaka kuyajua. Ikiwemo kuwakutanisha na watu ambao walitamani kukutana nao katika maisha yao. Jukumu la kuwaonyesha Daslama ikoje tulifanikiwa.

Ukitazama ulichonacho utahisi una ziada, ukitazama unachokosa hautokuwa na zaidi. Muda una kikomo, usiishi maisha ya mwingine. Maisha ni asilimia 10 ya upatacho, asilimia 90 ni kile unachokabiliana nacho. Maisha ni kile kinachokutatiza wakati unapangilia mikakati yako. ‘Fiesta haijatendewa haki.’