Alichokisema Lema kuhusu kugombea ubunge Arusha

Muktasari:

  • Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema amesema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 atawania ubunge katika jimbo hilo huku akitamba kuwa hakuna wa kumuondoa.

Arusha. Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema amesema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020 atawania ubunge katika jimbo hilo na si Hai kama ambavyo watu wengi wanazusha.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumapili Januari 6, 2019 Lema amesema kuna propaganda zinasambazwa kuwa haonekani jimboni kwake kwa kuwa anataka kuwania ubunge Hai ambako mbunge wake ni mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

“Hakuna wa kuniondoa ubunge wa Arusha Mjini. Kinachozungumzwa nakisikia ni vile tu nimeamua kubadili siasa zangu kwa kuacha kuwajibu maana kila wanapogombana na mimi wanapanda vyeo,” amesema Lema.

"Arusha tuna madiwani wachapakazi  na meya mzuri wanatosha kupambana na siasa za CCM Arusha. Mimi kama mbunge nijikite katika masuala ya kitaifa zaidi kwani kazi za maendeleo  zinasimamiwa vyema.”

Amesema mwaka 2019 utakuwa mwaka wa kupigania   ukombozi wa Watanzania wote, kwa kushirikiana na vyama vingine wamejipanga kudai Katiba Mpya, uhuru wa watu kuishi na kufanya shughuli zao  bila hofu.

"Leo maduka ya kubadilisha fedha yote yamefungwa Arusha, biashara zimefungwa, wawekezaji wanaondoka na hofu imetanda kila kona sasa mwaka huu ni wa kazi kurejesha matumaini kwa Watanzania,” amesema.

Alisema  taifa linapita katika wakati mgumu na zinahitajika hatua za haraka kuingilia kati ili viongozi warudi kwenye mstari, “Watu hawana matumaini tunafikiria kusaidia Watanzania.”