Tulia adai wabunge wanaosema hapana bungeni hawapendi maendeleo

Naibu Spika, Dk Tulia Ackson 

Muktasari:

Naibu Spika, Dk Tulia Ackson amesema wabunge wa CCM pekee ndio husema “ndiyo” bungeni ili kupitisha bajeti ya Serikali ikiwa ni ishara ya kuunga mkono maendeleo,  kudai wabunge wanaosema “hapana” hawapendi maendeleo

 


Dar es Salaam. Naibu Spika, Dk Tulia Ackson amesema wabunge wa CCM pekee ndio husema “ndiyo” bungeni ili kupitisha bajeti ya Serikali ikiwa ni ishara ya kuunga mkono maendeleo,  kudai wabunge wanaosema “hapana” hawapendi maendeleo.

Dk Tulia ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Januari 11, 2019 wakati wa kupokea ndege ya pili aina ya Airbus A220-300 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere(JNIA) jijini Dar es Salaam.

Amesema wanaokataa huwa hawapendi kuona mambo mazuri yanatendeka na wanashindwa kufurahia mazuri yanapofanyika.

“Tunaposema ndiyo tunamaanisha haya na wanaosema hapana wanapinga bila kujua manufaa yake,” amesema Dk Tulia

Kwa upande wake Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Tanzania haikutarajia kuwa na shirika la ndege lililo hai lenye idadi kubwa ya ndege kama ilivyo sasa.

“Tutaendelea kukusaidia (Rais John Magufuli) ili kufikia maono yako na uendelee kutupa maelekezo tutayafanyia kazi ili kuhakikisha lengo tunalitimiza,” amesema Majaliwa.

“Hii ni miaka mitatu na mpaka mitano tukiondoka tutakuwa tumetimiza ahadi zetu kwa asilimia 90. Niwapongeze ATCL kwa kazi kubwa mnayofanya.”