Wananchi Dodoma wafurahia gari la kubeba maiti

Muktasari:

Wenyeviti wa mitaa iliyopo katika Jiji la Dodoma wameshukuru mbunge wao kwa kuwapatiwa huduma ya gari la kubebea maiti.

Dodoma. Wenyeviti wa mitaa iliyopo katika Jiji la Dodoma wameshukuru kupatiwa  huduma ya gari la kubebea maiti, huku baadhi yao wakisema awali walilazimika kutumia mikokoteni inayovutwa na ng’ombe kubebe miili ya wapendwa wao.

Gari hilo la kubebea maiti lilitolewa na mbunge wa Dodoma Mjini, Anthony Mavunde na tangu imezinduliwa wiki iliyopita tayari watu kadhaa wamenufaika nayo.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mavunde ambaye pia ni Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Sera, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, alisema gari hilo ni sehemu ya ahadi zake alizozitoa kwa wananchi ili kuwaondolea shida na gharama.

Mwenyekiti wa mtaa wa Muungano kata ya Chawa, Stephen Mazunguni amesema wananchi wake wamefarijika kwa huduma hiyo inayotolewa na mbunge wao.

“Tulio wengi tunaokuja kupata huduma (Hospitali ya Mkoa) wengi wetu tuna vipato vya chini. Tunatarajia kukodi magari watu wanakuwa na michango mingi lakini kulingana na gari hilo mtu anajua akifiwa na mgonjwa wake hana cha kukagharamia,” amesema.

Alisema awali walilazimika kuchangisha ili kupatikana fedha za kukodi gari ta kubeba mwiili kutoka Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Dodoma, ambazo ni kati ya Sh75,000 na 120,000 kulingana na ukubwa wa gari.

“Wengi wetu tulikuwa tunaishia zahanati ya Chawa mara Hospitali ya Wilaya Chamwino Ikulu hata ikiwa imetokea bahati mbaya ni kiasi cha kwenda na mkokoteni wa kusukuma na ng’ombe,” amesema.

Naye mwenyekiti wa wenyeviti wa mitaa jimbo la Dodoma Mjini, Matwiga Wikama amesema gari hilo limekuwa ni faraja kubwa kwa wakazi wa Dodoma Mjini hasa wenye kipato cha chini.

“Jana (juzi) tu tumepata msiba katika mtaa wangu wa Karume, tumenufaika na huduma hii. Wananchi wangu wamefarijika kwa sababu wameokoa Sh250,000 ambazo wangetumia kukodisha gari kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa hadi nyumbani,” amesema.

Alisema awali iliwabidi wananchi kuchangishana wenyewe ili kupata fedha za kusafirisha miili ya ndugu zao, lakini sasa  wanapiga simu tu na kupata usafiri.