VIDEO: Watu 7 wanaotuhumiwa kwa ujambazi wauawa Mwanza

Muktasari:

  • Polisi mkoani Mwanza wamewaua watu saba wanaotuhumiwa kwa ujambazi usiku wa kuamkia leo.

Mwanza. Watu saba wanaodaiwa kuwa majambazi wameuawa katika mapambano ya kujibizana kwa risasi na askari polisi katika tukio lililotokea alfajiri ya kuamkia leo eneo la Kishili jijini Mwanza.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jonathan Shanna amethibitisha tukio hilo lililomwacha askari polisi mmoja akijeruhiwa.

Akizungumza na Mwananchi katika eneo la tukio, diwani wa kata ya Kishiri, Sospeter Ndumi alilipongeza jeshi la polisi kwa kufanikiwa kudhibiti matukio ya kihalifu yanayotishia maisha na usalama wa wakazi wa kata hiyo inayoshuhudia makabiliano ya mara kwa mara kati ya polisi na makundi yanayoaminika kuwa ya kihalifu.

Makabiliano kati ya polisi na watuhumiwa hao wa ujambazi yalitokea mtaa wa Ihushi kata ya Kishili.

Kabla kutokea makabiliano ya kurushiana risasi, polisi walifanikiwa kumtia mbaroni mtuhumiwa mmoja ambaye ndiye aliwaongoza hadi kwenye maficho yao na kuwakurupusha wengine ambao badala ya kujisalimisha walianza mashambulizi ya risasi yaliyojibiwa na polisi.

Mwaka 2016, wakazi wa mtaa Fumagila kata ya  Kishiri walishuhudia makabiliano ya kurushiana risasi kati ya askari polisi na watu waliotuhumiwa kuwa ni majambazi. Watuhumiwa sita waliuawa kwa kupigwa risasi katika tukio hilo.