Kupatikana Mo kumeleta mzuka wachezaji Simba

Muktasari:

Kitendo cha kurejea akiwa salama mfanyabiashara na mwanamichezo maarufu nchini Mohammed Dewji ‘Mo’ kumerejesha morari na mzuka wa hali ya juu kwa wachezaji wa Simba ambao watashuka dimbani kesho kuikaribisha Stand United ya Shinyanga

Dar es Salaam. Baada ya kuwa na hali ya wasiwasi kwa siku tisa, wachezaji wa klabu ya Simba sasa wamerejea katika hali yao ya kawaida baada ya kupatikana salama kwa mdhamini wao, Mohammed Dewji maarufu kwa jina la Mo.

Dewji ambaye aliyetekwa Oktoba 11 mwaka huu alipatikana usiku wa leo kwenye viwanja vya Gymkhana jijini Dar es Salaam akiwa salama.

Mratibu wa klabu ya Simba, Abbas Ally alisema kuwa mara baada ya kupokea taarifa za kupatikana kwa Dewji, wachezaji walilipuka kwa furaha baada ya kuwa katika hali ya sintofahamu kwa siku tisa.

“Ni faraja kwetu wana Simba na wadau wa soka kwa ujumla, mbali kwa wadau na wana Simba, ni faraja pia kwa Watanzania ambao walifanya maombi kumwombea kwa Mungu mara baada ya kutekwa,” alisema Abbas.

Alisema kuwa ilifikia hatua ya kuhairisha mazoezi baada ya Mo kutekwa kwani wachezaji walikumbwa na taharuki.

“Tunawashukuru wote waliofanya jitihada za kupatikana kwa mfadhili wetu ambaye amechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya klabu mpaka sasa,” alisema.

Alifafanua kuwa mchezo wao dhidi ya Stand United itakuwa na msisimko wa aina yake kwani wachezaji hawatakuwa na jambo linguine wanalowazia zaidi ya kusaka ushindi.