LHRC yataka polisi kubadili mbinu

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga

Muktasari:

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga amesema kuwa Jeshi la Polisi badala ya kutumia mbinu za zamani wanachotakiwa kufanya ni kuwa na mafunzo ya kutosha, kufanya uchunguzi na kubaini wanatakiwa kufanya nini wakati gani na eneo gani.

Dar es Salaam. Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu (LHRC) kimelitaka Jeshi la Polisi kubadili mbinu za kukabiliana na uhalifu kwa sababu mbinu wanazotumia sasa zimekuwa zikiwasababishia usumbufu wananchi wasiokuwa na hatia.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga amesema kuwa Jeshi la Polisi badala ya kutumia mbinu za zamani wanachotakiwa kufanya ni kuwa na mafunzo ya kutosha, kufanya uchunguzi na kubaini wanatakiwa kufanya nini wakati gani na eneo gani.

Amesema hivi sasa hata wahalifu wamebadili mbinu za kufanya uhalifu, hivyo wao wakiendelea kutumia mbinu zile zile itakuwa ngumu kuwabaini na matokeo yake watawaingiza waliokuwamo na wasiokuwamo.

Amefafanua kuwa kituo kinaendelea kufuatilia kwa ukaribu mwenendo na haki za binadamu nchini na kubaini kuongezeka kwa vitendo vya mauaji yanayotokana na wananchi kujichukulia sheria mkononi na yanayofanywa chini ya vyombo vya dola.

Ameeleza katika taarifa yao ya mwaka 2016 wamebaini kuwapo kwa mauaji yatokanayo na wananchi kujichukulia sheria mikononi kuwa 705 na yaliyofanyika chini ya vyombo vya dola kuwa manne.