Lissu: Tumeshinda, tumeshashinda

Muktasari:

  • Lissu ambaye ni mwanasheria wa Chadema ametimiza siku 13 tangu alazwe katika Hospitali ya Nairobi (Nairobi Hospital) na hali yake inaendelea vizuri baada ya kushambuliwa na kujeruhiwa kwa risasi Septemba 7, nyumbani kwake Area D mjini Dodoma.

Dar es Salaam. “Tumeshinda. Tumeshashinda.” Hayo ni maneno aliyoyatamka Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu akimweleza Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe aliyekwenda kumjulia hali jijini Nairobi, Kenya.

Lissu ambaye ni mwanasheria wa Chadema ametimiza siku 13 tangu alazwe katika Hospitali ya Nairobi (Nairobi Hospital) na hali yake inaendelea vizuri baada ya kushambuliwa na kujeruhiwa kwa risasi Septemba 7, nyumbani kwake Area D mjini Dodoma.

Baada ya kumuona Lissu, Zitto ambaye ni Kiongozi wa ACT-Wazalendo alitumia mitandao ya kijamii hasa ukurasa wa Facebook kuandika kwa kuanza na kichwa cha habari ‘Ujasiri’ kisha akaendelea kuandika, “Nimetumia wikiendi iliyopita kumsabahi ndugu Lissu Nairobi. Nimerudi nikiwa mwenye unyenyekevu zaidi kwa sababu ya nguvu na ujasiri ambao kaka yangu ameuonyesha licha ya kuwa yupo kwenye maumivu makali.”

“Si mara nyingi hapa nchini utasikia tukiongelea ujasiri. Lakini namfikiria Lissu na vile nilivyojisikia nikiwa pamoja naye Nairobi. Najua hivyo ndivyo alivyo. Waliomshambulia wamemuumiza. Wamemuumiza kweli. Na bado wakati tuliokuwa naye amenionyesha shukrani, ari na ucheshi. Huo ni ujasiri.”

Zitto aliendelea kwa kuandika kuwa, “alichopitia na anachoendelea kupitia Lissu siyo kitu rahisi kwa mtu yeyote, kutafakari na kufikiria hali ile kungeniacha nimeumia moyo kama asingesema maneno haya kwangu: ‘Tumeshinda Tumeshashinda’.”

Mbunge huyo alimalizia kwa kuandika, “ujasiri ni Lissu.”

Wakati Zitto akiandika hayo, juzi wabunge na meya wa Chadema walifanya ibada ya kumuombea Lissu iliyofanyika jijini Nairobi katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri. Waliohudhuria ibada hiyo ni Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, John Heche (Tarime Vijijini), Joshua Nassari (Arumeru Mashariki), Godbless Lema (Arusha Mjini) na Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita.

Baada ya kumalizika ibada hiyo, Mchungaji Msigwa aliwashukuru wote walioonyesha mapenzi mema kwa Lissu na kwa Chadema na kutoa wito kwa Watanzania kuendelea kumuombea mwanasiasa huyo na kutoa michango.

Wakati Mchungaji Msigwa akieleza hayo, Lema alisema wakati huu umekuwa wa hofu, hivyo aliwasihi watu wote wa Afrika Mashariki kumuomba Mungu aiondoe akigusia pia uchaguzi Mkuu wa Kenya.

Kwa upande wake, Mwita ambaye pia Diwani wa Vijibweni (Kigamboni), alisema wananchi wana kazi ya kumuombea Lissu ili apone aweze kuendeleza mapambano ya kuwatetea.

Mbali na viongozi hao wa Chadema na Zitto, wengine waliokwenda kumuona Lissu ni Jaji Mkuu mstaafu, Mohamed Chande Othman na Mbunge wa Singida Kaskazini (CCM), Lazaro Nyalandu.

Baada ya kumjulia hali, Nyalandu alisema Lissu alionyesha uso wa tabasamu, huku akimshukuru Mungu kwa kumruhusu kuwa hai.

Nyalandu alieleza hayo kwa kutumia ukurasa wake wa Facebook kama ilivyo kwa Zitto akiandika,“Muda mfupi uliopita nimeonana na Mh Lissu katika chumba chake hospitali ya Nairobi na kuzungumza naye kuhusu hali yake na anavyoendelea.”

“Ukweli ni kwamba ameumizwa vibaya. Imeelezwa kwamba madaktari wanaendelea na hatua kadhaa za matibabu, wakiwa wameanza kwa kumuimarisha (stabilization), ili kuufanya mwili uweze kumudu hatua zaidi za utabibu anazopaswa kufanyiwa.”

Nyalandu ambaye aliwahi kuwa Waziri wa Maliasili na Utalii katika Serikali ya Awamu ya Nne alisema anaamini hatua zaidi na za haraka zitahitajika kumsaidia ili apate huduma haraka za kitabibu katika ubora na ufanisi uliopo kwa sasa duniani.

Wakati wabunge wa Chadema wakipata fursa ya kumuombea Lissu jijini Nairobi, hapa nchini Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha) lilikwama kufanya maombi yaliyopangwa kufanyika kwenye viwanja vya TP-Sinza baada ya polisi kufanikiwa kuzuia mchakato huo.

Mbali na hilo, polisi iliwashikilia vijana watano kwa mahojiano wakidaiwa kutaka kuandaa maombezi yaliyopigwa marufuku kwenye uwanja huo.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Murilo Jumanne aliwaambia wanahabari kwamba wenye nia ya dhati ya kufanya maombi au kuabudu wapo katika makanisa na misikitini na siyo katika uwanja huo.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Bavicha, Patrobas Katambi alisema waliamua kufanya maombi katika uwanja huo ili kuwapa fursa watu wa dini zote kujumuika.

“Hatukupanga kumuombea Lissu peke yake, bali watu mbalimbali ikiwamo yule meja jenerali mstaafu aliyeshambuliwa kwa risasi hivi karibuni. Pia kuliombea Taifa kwa ujumla kutokana na vitendo vinayofanywa na watu wasiojulikana,” alisema Katambi.

Mamilioni ya matibabu

Wakati hayo yakitokea watu mbalimbali wameendelea kuchanga fedha kusaidia matibabu ya Tundu Lissu.

Michango hiyo inatolewa baada ya Chadema kuomba msaada kwa yeyote anayeguswa ili kuhakikisha Lissu anapata matibabu bora.

Makamu Mwenyekiti wa Chadema Tanzania Bara, Profesa Abdallah Safari hivi karibuni alieleza kuwa gharama za matibabu ya mbunge huyo ni Sh10 milioni kwa siku. Hadi jana jioni kwenye uchangishaji unaofanyika kwa njia ya mtandao zilikuwa zimefikia takriban Dola18,000 za Marekani (sawa na zaidi ya Sh39 milioni).

Mbali na hilo, taarifa kutoka chanzo chetu kinachoaminika kilieleza kuwa Chadema wamepata mchango wa Dola30,000 za Marekani kutoka nje ya nchi ambazo ni sawa na Sh66 milioni.

Sugu atumia msiba kumuombea

Katika mazishi ya Diwani wa Viti Maalumu Mbeya Mjini (Chadema), Ester Mpwiniza, mbunge wa jimbo hilo, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ alimuomba marehemu akamuombee kwa Mola mwanasheria mkuu wa chama hicho, Lissu ili aweze kupona haraka.

Sugu alitoa maneno hayo jana jioni wakati akielezea sifa na wasifu wa Mpwiniza ambaye aliwahi kuwa mwenyekiti wa Baraza la Wanawake (Bawacha) Mbeya Mjini, alipokuwa akitoa salamu zake kabla ya kufanyika kwa mazishi kwenye makaburi ya Sabasaba jijini hapa.

Alisema anakipeleka kilio hicho kwa Mungu kwa kuwa hali ya nchi ilipofikia sasa si salama akidai upinzani umekuwa ukipata vikwazo vingi hata pale wanapofanya maombi ya pamoja, kujiombea na kuiombea nchi amani wanazuiwa.

Pia, alisema licha ya kuwa Mpwiniza alikuwa ngao kubwa katika ulingo wake wa kisiasa, pia anaamini huko aendako atapokewa na malaika kutokana na kuyaishi maisha ya upendo, ujasiri na kuwa mwanamke aliyethubutu kuwaunganisha wenzake.

“Nakuomba dada yangu Ester naamini huko mbinguni umekwishapokelewa na malaika, nakuomba dada nenda kwa Mungu muombe asimamie uhai wa Tundu Lissu, amlinde na aponye haraka majeraha yake yaliyosababishwa na shambulio la risasi. Mungu akuongoze kwenye sala,” alisema Sugu.

Mbali na hilo, Sugu alitoa sifa kwa Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson aliyehudhuria msiba huo bila kujali itikadi ya chama chake cha siasa na kuonyesha dhahiri alivyo na mapenzi na ndugu zake wa Mkoa wa Mbeya.

Alisema kuwa Dk Tulia alionyesha ukomavu wa kisiasa na kwamba, hizo ni salamu tosha za kupeleka kwenye mamlaka nyingine ambazo badala ya kuwaunganisha wananchi katika misiba, zinasababisha watu wengine waogope kuzikana wakati kifo hakina itikadi.