Lowassa akanusha taarifa za kuomba kurejea CCM

Muktasari:

Waziri mkuu huyo mstaafu amezungumzia kuhusu taarifa zinazoenea kuwa ameomba kurudi CCM

Arusha. Waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa amesema hana mpango wa kurejea CCM kama ambavyo taarifa zimekuwa zikisambazwa kwenye mitandao ya kijamii.

Akizungumza na Mwananchi  leo Jumanne,  Lowassa amesema amepata taarifa za uvumi unaosambazwa kuwa kuna watu amewatuma kuomba arudi CCM jambo ambalo ni uongo.

"Huu ni uongo wa kutunga, wamekuwa wakitunga vitu vingi juu yangu, mimi sina mpango wa kurejea CCM," amesema Lowassa,ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema  . 

Amesema uongo mwingine ambao unasambazwa ni kuwa Serikali imezuia watu kumtembelea nyumbani kwake jambo ambalo anaamini ni maneno yanayotungwa.

"Watu wanazuiwa kuja nyumbani kwangu, eti Serikali imezuia hivyo wanakuwa wanaogopa huu ni uongo Serikali haiwezi kuzuia watu kutembeleana," amesema.