Lugola awashukia uhamiaji, awataka wajitathimini

Kamishna jenerali wa uhamiaji Dk Anna Makakala akizungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Kangi Lugola aliyefika idara ya uhamiaji jijini Dar es salaam wakati wa ziara ya kikazi.

Muktasari:

Amesema utendaji wa idara ya uhamiaji hauridhishi.

Dar es Salaam. Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Kangi Lugola amewataka askari wa uhamiaji waliopo mipakani

kujitafakari kwa maelezo kuwa utendaji wao hauridhishi.

Akizungumza leo Alhamisi Julai 12, 2018 katika kikao cha watendaji wakuu wa uhamiaji alipotembelea makao makuu ya idara ya uhamiaji, Lugola amesema ametoa kauli hiyo kutokana na wahamiaji haramu kuingia nchini, wakipitia maeneo ya mipakani.

Amesema ni ajabu kuona wahamiaji hao wakipakiwa katika magari na kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine bila kukamatwa.

“Tatizo liko wapi, inakuaje magari yaliyobeba wahamiaji yanatokea mpaka wa Himo (Kilimanjaro), yanapita Arusha na Manyara yanakwenda kukamatwa Dodoma?” amehoji.

“Uhamiaji mnakuwa wapi? Inasikitisha watu hawa wanapita mikoa hiyo bila kukamatwa. Watu wa mipakani wajitafakari sana hatuwezi kukubali hali hii.”

Amemtaka Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dk Anna Makakala kutowatetea askari wasiotekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

"Tutawatetea na kuwalinda askari wanaofanya kazi zao sawasawa na tukiona mtu anataka kuwaonea tutapambana naye,"amesema

Lugola pia amezungumzia jinsi watu wanavyomchukulia, akibainisha kuwa wapo wanaomuona kuwa chakalamu na kubainisha kuwa atahakikisha anawakimbiza watendaji wa idara za wizara hiyo ili kutenda kazi zao kwa ufanisi.

Amesema anafanya hivyo kwa kuwa wizara hiyo haijasemwa kwa mazuri na Rais John Magufuli.

Lugola amesisitiza suala la rushwa, kumuagiza Dk Makalala kuliangalia jambo hilo ndani ya watendaji wa idara hiyo.