MAT wataka uchunguzi tukio la daktari kupigwa na polisi

Rais wa chama Chama cha Madaktari Tanzania  Dk Obadia Nyongole 

Muktasari:

Taarifa ya MAT imezitaka mamlaka husika kuchukua hatua kali kwa wote waliohusika na unyama huo.  

Dar es Salaam. Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), kimelitaka Jeshi la Polisi kuchunguza na kuweka taarifa sahihi kuhusu tukio la kushambuliwa na polisi kwa Mkuu wa Kituo cha Afya cha Katoro, Geita Dk Peter Janga.

Katika taarifa iliyotolewa na MAT leo Juni 13, na kusainiwa na Rais wa chama hicho Dk Obadia Nyongole, Dk Janga alishambuliwa na polisi akiwa kazini Juni 6 mwaka huu.

“Chama cha Madaktari Tanzania tunatoa pole kwa daktari na watumishi wenzake kwa kitendo dhalimu kilichofanywa na jeshi la polisi wilayani geita. Tunaomba mamlaka husika kufanya uchunguzi wa wazi na shirikishi ili kuweka taarifa sahihi,” imesema taarifa hiyo

 Kadhalika taarifa ya MAT imezitaka mamlaka husika  kuchukua hatua kali kwa wote waliohusika na unyama huo. 

“Tunawaomba madaktari kuwa watulivu wakati huu mgumu kwa mwenzetu huku tukiendelea kufuatilia kwa karibu tukio hili.” Imesema taarifa hiyo