Maafa mengine Rukwa, nyumba 21 zabomoka

Muktasari:

Mbali na kuharibu nyumba hizo na kuacha familia bila makazi, mvua hiyo imeua  mbuzi wanane, nguruwe mmoja na kuku zaidi ya 100.

Rukwa. Nyumba 21 zimebomoka baada ya mvua ya mawe iliyoambatana na upepo mkali kunyesha katika Kijiji cha Mtimbwa, Kata ya Kisesa wilayani Sumbawanga.

Mbali na kuharibu nyumba hizo na kuacha familia bila makazi, mvua hiyo imeua mbuzi wanane, nguruwe mmoja na kuku zaidi ya 100.

Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Mtimbwa, Wilbroad Kapufi alisema mvua hiyo iliyonyesha kwa nusu saa kuanzia saa 11:00 alfajiri jana, ilisababisha taharuki kubwa kijijini hapo.

“Tumepita maeneo mbalimbali ili kushuhudia athari iliyosababishwa na mvua hiyo na kubaini nyumba 21  zimebomolewa na nyingine zimeezuliwa mapaa ila hakuna kifo  kilichotokea,  lakini watoto watatu walinusurika kifo baada ya kusombwa na mafuriko wakiwa shambani,  wote  waliokolewa na kupewa matibabu na hali zao ni nzuri,” alisema.