Maalim Seif atangaza adui wake wa nne

Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad akizungumza kwenye mkutano na wandishi wa habari, jijini Dar es Salaam jana. Picha na Omar Fungo

Muktasari:

  • Adui wa kwanza wa CUF baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa 2015 alikuwa mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, kisha mwenyekiti wa chama chake, Profesa Ibrahim Lipumba kabla ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kuingia kwenye orodha hiyo.

Dar es Salaam. Baada ya kuingia katika mgogoro na viongozi wa taasisi tatu tofauti, katibu mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad sasa ameitangazia vita ofisi ya Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (Rita).

Adui wa kwanza wa CUF baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa 2015 alikuwa mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, kisha mwenyekiti wa chama chake, Profesa Ibrahim Lipumba kabla ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kuingia kwenye orodha hiyo.

Maalim Seif aliingia katika mgogoro na Jecha baada ya mwenyekiti huyo wa ZEC kufuta matokeo ya Uchaguzi Mkuu Zanzibar mwaka 2015 wakati wananchi wakisubiri kutangazwa kwa matokeo ya urais, siku ambayo alitakiwa kutangaza mshindi kiti cha urais.

Jecha alitangaza hatua hiyo wakati matokeo ya majimbo 31 yakiwa yameshatangazwa, huku matokeo ya majimbo tisa yakiwa yameshahakikiwa na kusubiri kutangazwa. Pia washindi wa viti vya uwakilishi walishatangazwa na kupewa hati za ushindi.

Jecha alitangaza uchaguzi huo kurudiwa Machi 20, 2016, lakini CUF wakasusia.

Naye Profesa Lipumba aligeuka adui baada ya kujiuzulu uenyekiti na nyadhifa nyingine zote kabla ya kubadili uamuzi huo baada ya mwaka mmoja, jambo ambalo linapingwa na mkutano mkuu ukiongozwa na Maalim Seif.

Lakini, Jaji Mutungi akatangaza kumtambua na hivyo kujikuta akiwa adui wa tatu wa chama hicho.

Sasa, Rita ambayo imeitambua Bodi ya Wadhamini iliyoundwa na Profesa Lipumba, amegeuka kuwa adui mwingine.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Maalim Seif alisema Rita imetimiza nia yake ovu ya kusajili kinyume cha taratibu bodi aliyoiita “feki” ya wadhamini ya upande wa Profesa Lipumba na kudai kuwa kwa taarifa alizonazo na zisizo na shaka, hatua hiyo imetokana na shinikizo kubwa alilopata ofisa mtendaji mkuu wa taasisi hiyo kusajili wajumbe wa bodi hiyo.

Ametoa kauli hiyo siku chache baada ya Ofisa Mtendaji Mkuu wa Rita, Emmy Hudson kukaririwa akisema kuwa aliisajili bodi hiyo mpya baada ya kupata uthibitisho kutoka kwa Msajili wa Vyama vya Siasa kuwa anautambua uongozi wa Profesa Lipumba.

Lakini jana, Maalim Seif aliyeambatana na viongozi wanaomuunga mkono, aliwaeleza wanahabari kuwa utetezi huo haumuondolei Hudson tuhuma za matumizi mabaya ya madaraka, akisema anayesajili bodi si Msajili wa Vyama vya Siasa, bali ni Rita na sheria inataka kujiridhisha na nyaraka zinazowasilishwa ofisini kwake na waombaji.

“Aprili 9 mwaka huu, nilitoa maelezo ya kutosha kuhusu mbinu chafu iliyopangwa kufanywa na Rita kwa maelekezo ya dola kupitia Msajili wa Vyama vya Siasa kwa lengo la kumnusuru Profesa Lipumba na nilifafanua kwa kina hujuma zinazofanywa dhidi ya CUF.,” alisema Maalim Seif.

“Niseme tu yale niliyoyaeleza leo yametimia na yamethibitika wiki iliyopita kwa Rita kutekeleza walichoagizwa kufanywa ambacho ni kusajili wajumbe feki wa bodi ya wadhamini.”

Maalim Seif alidai kwamba nyaraka mbalimbali za wajumbe wa bodi zimeghushiwa na kwamba kwa kawaida majina hayo huteuliwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa lakini yaliyopelekwa Rita hayakupita huko.

Alisema Baraza Kuu la Uongozi lililochaguliwa kihalali kupitia Mkutano Mkuu wa 2014 kwa kufuata masharti mapya ya Katiba 1992 (Toleo la 2014), lilifanya mabadiliko machache ya wajumbe wa bodi ya wadhamini Machi 2017 na kuyawasilisha kupitia barua ya katibu mkuu ambayo yalipokewa na Rita.

Maalim Seif ambaye alikuwa Makamu wa Kwanza wa Rais katika Serikali iliyopita ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK), alidai kuwa baada ya kugundua kuwa chama kina nakala halisi na stakabadhi za malipo hadi mwaka 2016 na nyaraka zao za kughushi hazina nafasi, Profesa Lipumba na wenzake waliamua kuja na njama ya kusajili bodi feki ili watekeleze majukumu yao kwa ufanisi.

Alisema wamegundua mambo manne ambayo upande wa Profesa Lipumba umedhamiria kufanya ikiwamo kufuta kesi zote zilizofunguliwa.