Maaskofu KKKT watoa waraka mzito wa Pasaka

Muktasari:

Katika ujumbe huo maaskofu wamegusia masuala makuu matatu ambayo ni jamii na uchumi, maisha na siasa.


Dar es Salaam. Maaskofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) wametoa waraka mzito wa Sikukuu ya Pasaka.

Ujumbe huo uliosainiwa na maaskofu 27 wa KKKT waliokutana Machi 15, 2018 umepangwa kusomwa kesho Machi 25, 2018 katika makanisa yote nchini.

Akizungumza na Mwananchi leo Machi 24, 2018 Askofu wa Dayosisi ya Karagwe mkoani Kagera, Benson Bagonza amesema, "Ni ujumbe wa Pasaka ambao utasomwa kesho kwa washirika wetu makanisani."

Katika ujumbe huo maaskofu, wamegusia masuala makuu matatu ambayo ni jamii na uchumi, maisha na siasa na mambo mtambuka yanayohusiana na hayo ikiwemo demokrasia, huku wakisisitiza Katiba mpya ya wananchi ni suluhu ya yote.

Ujumbe huo umegusia masuala ya wanasiasa kuhama chama kimoja na kwenda kingine pamoja na mabadiliko ya mara kwa mara ya mfumo wa elimu kwamba una athari kwa Taifa.