Madini mengine si yetu kisheria-Lissu

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Tundu Lissu (kushoto) akizungumza na waandishi waandamizi na wahariri wa gazeti la Mwananchi alipotembelea ofisi za Mwananchi Communications Limited (MCL) zilizopo Tabata, jijini Dar es Salaam jana. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

  • Lissu amesema kwa maoni yake Serikali haipaswi kuzuia madini hayo kusafirishwa kwenda nje kwa kuwa ni kukiuka mikataba na sheria ya madini.
  • “Hili halizungumzwi kabisa na liko katika mikataba. Madini mengine si yetu kwa sababu haihesabiwi katika asilimia mia ya dhahabu,” amesema mwanasheria huyo wa kujitegemea alipotembelea ofisi za Mwananchi.

Dar es Salaam. Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu amezungumzia sakata la makontena ya mchanga unaodaiwa kuwa na madini uliozuiwa katika Bandari ya Dar es Salaam, akisema madini mengine yaliyomo humo siyo mali ya Tanzania.

Lissu amesema kwa maoni yake Serikali haipaswi kuzuia madini hayo kusafirishwa kwenda nje kwa kuwa ni kukiuka mikataba na sheria ya madini.

“Hili halizungumzwi kabisa na liko katika mikataba. Madini mengine si yetu kwa sababu haihesabiwi katika asilimia mia ya dhahabu,” amesema mwanasheria huyo wa kujitegemea alipotembelea ofisi za Mwananchi.

Mbunge huyo amesema kwamba, kwa hoja za kodi Taifa halina chake katika suala la madini, isipokuwa ni asilimia nne ya pato inayolipwa na mwekezaji kama mrahaba kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya mwaka 1998.

 Lissu ameongeza kuwa sheria hiyo inampa mamlaka mwekezaji kuwa, iwapo anapatiwa leseni ya uchimbaji kile anachopata ardhini kinakuwa ni mali yake.

“Haki yetu ni asilimia nne tu ya mirabaha. Kwa kifupi, kwenye madini tumewapa (wawekezaji) madini bure, tena kisheria,” amesema.

Mwanasiasa huyo amesema anashangaa kuona mchanga unazuiwa bandarini wakati Rais John Magufuli alikuwa katika Baraza la Mawaziri wakati Sheria ya Madini ya mwaka 1998 na 2010 zikipitishwa.