Madiwani 19 waliotimka Chadema, kugombea tena kupitia CCM

Katibu mwenezi wa CCM Mkoa wa Arusha,  Shaban Mdoe

Muktasari:

wagombea hao wamepitishwa na wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM mkoa wa Arusha katika kikao chao kilichofanyika leo Alhamisi Julai 12, 2018

Arusha. Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha kimetangaza majina ya wagombea wa udiwani katika Kata 20, huku 19 kati yao wakiwa ni wale waliokuwa madiwani wa kata hizo kwa tiketi ya Chadema kabla ya kujiuzulu na kujiunga na chama hicho tawala.

Uchaguzi wa madiwani katika kata 79 pamoja na ubunge katika jimbo la Buyungu utafanyika Agosti 12, 2018.

Akizungumza leo Katibu mwenezi wa CCM Mkoa wa Arusha,  Shaban Mdoe amesema wagombea hao wamepitishwa na wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM mkoa wa Arusha katika kikao chao kilichofanyika leo Alhamisi Julai 12, 2018.

Baadhi ya madiwani hao ni pamoja na wanne wa halmashauri ya jiji la Arusha.

Nao  ni Prosper Msoffe anayewania udiwani kata ya Daraja mbili. Msoffe amewahi kuwa Naibu Meya wa jiji la Arusha kwa tiketi ya Chadema. Wengine ni  Elirehema Nnko (Osunyai), Obed Men’goriki (Terati) na Emanuel Kessy (Kaloleni).