Magufuli atoa neno ajira za wazawa

Muktasari:

  • Rais Magufuli ataka ajira kwa wazawa viwandani akisema ndio waliompigia kura.

Rais John Magufuli amemwagiza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage kuhakikisha wamiliki wa viwanda vya ndani wanaajiri wazawa.

Ametoa agizo hilo leo Jumapili Machi 11,2018 akizindua kiwanda cha kufua vyuma cha Kahama Oil Mill mjini Kahama mkoani Shinyanga.

Rais amesema wananchi wazawa ndio waliompigia kura, hivyo wapewe kipaumbele cha ajira katika viwanda hivyo.

“Kama wewe ni waziri nimekuteua mimi, unaacha kuwaajiri wazawa walionipigia kura unaenda kuchukua watu wa nje hii hakubaliki,” amesema.

Rais Magufuli amesema, “Nitoe wito kwa mawaziri wangu na wakurugenzi, hakikisheni viwanda mnavyovianzisha nchini mnaajiri Watanzania, hawa ndio walionipigia kura.”

Amewataka wamiliki wa viwanda kuhakikisha wanatumia malighafi za ndani kutengeneza bidhaa badala ya kuagiza kutoka nje ya nchi.

“Mwaka huu pamba nyingi imelimwa, Kahama Oil Mill pia mnatengeneza mafuta, hakuna haja ya kuagiza pamba kutoka nje wakati tuna pamba ya kutosha hapa,” amesema.

Kuhusu kiwanda cha chuma amesema malighafi inapatikana nchini, hivyo iwapo mkurugenzi wa Kahama Oil Mill anahitaji yupo tayari kumpa bure badala ya kuagiza nje.

Pia, amewataka Watanzania kununua bidhaa za ndani, huku akiwataka wamiliki wa viwanda kutengeneza zenye ubora ili kuhimili ushindani.