Magufuli awapa ‘makavu’ wabunge

Rais John Magufuli

Muktasari:

  • Mbali ya kumkingia kifua Majaliwa, Mwenyekiti huyo wa CCM pia amewaonya wabunge wa chama hicho wanaotoa muda wao wa kuchangia bungeni kwa wapinzani, huku akieleza kukerwa na wabunge wanaofifisha vita dhidi ya dawa za kulevya na mmoja akimtuhumu kutoa siri za chama kwa upinzani.

Dodoma. Rais John Magufuli amewapasulia jipu wabunge wa CCM kuwa anamuunga mkono Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa hata kama wapo miongoni mwao wanaompinga.

Mbali ya kumkingia kifua Majaliwa, Mwenyekiti huyo wa CCM pia amewaonya wabunge wa chama hicho wanaotoa muda wao wa kuchangia bungeni kwa wapinzani, huku akieleza kukerwa na wabunge wanaofifisha vita dhidi ya dawa za kulevya na mmoja akimtuhumu kutoa siri za chama kwa upinzani.

Rais Magufuli aliyekutana jana na wabunge hao Ikulu ndogo ya Chamwino mjini hapa, pia aliwaambiwa kwamba yeye ndiye aliyeamua kusitisha mikutano ya Bunge kuonyeshwa moja kwa moja katika televisheni.

Kikao hicho cha ndani kimefanyika siku moja baada ya kumalizika kwa Mkutano Mkuu wa CCM mjini hapa na kupitisha mageuzi makubwa ya kikatiba na kanuni kwa chama hicho tawala.