VIDEO: Maiti ajali MV Nyerere zaanza kutambuliwa

Muktasari:

Shughuli ya kutambua miili ya waliofariki dunia baada ya kivuko hicho  kuzama katika Ziwa Victoria jana limeanza leo

Dar es Salaam. Shughuli ya kutambua miili ya waliofariki dunia baada ya kivuko cha MV Nyerere kuzama katika Ziwa Victoria jana imeanza leo.

Ndugu na jamaa wa waliopoteza wapendwa wao katika ajali hiyo wameanza kufika eneo lilihifadhiwa miili hiyo kwa ajili ya utambuzi.

Kivuko hicho kilizama jana katika Ziwa Victoria mita 50 kabla ya kutia nanga kisiwa cha Ukara.

Kilikuwa kikitokea katika kisiwa cha Bugolora kuelekea kisiwa cha Ukara wilayani Ukerewe kikidaiwa kilikuwa kimepakia zaidi ya abiria 100, wengi wakiwa wanaelekea kwenye gulio.

Akizungumza katika eneo hilo leo, Mkuu wa Jeshi la Polis, Inspekta Jenerali, Simon Sirro alisema  utambuzi huo unasimamiwa na maofisa wa Serikali.

Alisema wananchi wengi wameonyesha ushirikiano na ana amini kazi ya kutambua miili hiyo itaendelea kufanyika katika hali ya utulivu.

“Wananchi wa eneo hili wameonyesha ushirikiano mkubwa na tangu kutokea kwa tukio hili wengi wameendelea kujitokeza wakitoa msaada unaohitajika,” alisema katika mkutano wake na waandishi a habari uliorushwa moja kwa moja hewani na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).