Majaliwa: Serikali inahitaji wafanyabiashara

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

Arusha. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali inahitaji ushirikiano mkubwa na wafanyabiashara, hivyo haitakubaliana na mtumishi yeyote wa umma atakayefanya urasimu kwa lengo la kukwamisha uboreshaji wa sekta binafsi.

Amesema miongoni mwa maboresho yanayofanywa na Serikali katika sekta binafsi ni pamoja na kuimarisha utendaji wa watumishi na kuondoa urasimu katika utendajikazi wa kila siku baada ya eneo hilo limelalamikiwa sana.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo jana jioni (Ijumaa, Desemba 2, 2016) wakati akizungumza na wafanyabiashara, wamiliki wa viwanda mkoani Arusha kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC) akiwa katika siku ya kwanza ya ziara ya kikazi mkoani Arusha.

Ziara hiyo inalenga kuangalia utelelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM,Utendaji wa Serikali, kusikiliza na kujionea kero zinazowakabili wananchi  wa Mkoa huo na kushirikiana na viongozi wa Mkoa ili kuweza kuzipatia suluhisho.

“Serikali inafanya jitihada kubwa katika kuhakikisha inaweka mazingira mazuri ya uwekezaji ili kukuza uchumi wa nchi yetu. Pia mapambano dhidi ya rushwa yanayofanyika ndani ya Serikali na nje yanalenga kuleta maboresho makubwa katika sekta binafsi ,” alisema.