Majaliwa aagiza “beacons” ziwekwe kwenye hifadhi za misitu

Waziri Mkuu,  Kassim Majaliwa

Muktasari:

Majaliwa ametoa agizo hilo leo (Jumatatu) wakati akizungumza na watendaji wakuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii na wakuu wa mapori ya Hifadhi za Misitu nchini katika kikao alichokiitisha kwenye ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma.

Dar es Salaam. Waziri Mkuu,  Kassim Majaliwa ametoa miezi miwili kwa wakuu wa Mapori ya Hifadhi za Misitu kuhakikisha wanaweka mawe ya alama (beacons) kwenye mipaka yao ili kuepusha migogoro na wanavijiji wanaowazunguka.

Majaliwa ametoa agizo hilo leo (Jumatatu) wakati akizungumza na watendaji wakuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii na wakuu wa mapori ya Hifadhi za Misitu nchini katika kikao alichokiitisha kwenye ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu mjini Dodoma.

Waziri Mkuu amesema migogoro baina ya wafugaji, wakulima na kamati za ulinzi na usalama za mikoa na wilaya ni lazima zifanyiwe kazi.

“Mkitoka hapa rudini katika maeneo yenu mkawaambie wananchi mipaka yenu iko wapi. Ninyi mnatambua mipaka yenu iko wapi kwa hiyo waelewesheni wananchi kwa kuweka alama.

“...Sasa ninawapa muda hadi Januari 31, 2017 kazi ya kuweka beacons kwenye hifadhi zote za misitu iwe imekamilika. Kila pori nenda mkatengeneze alama zenu kama TANROADS walivyofanya. Kaeni mpige hesabu ni kiasi gani cha saruji na kokoto kinahitajika. Tutarudi hapa Dodoma kupeana taarifa ya utekelezaji. Katibu Mkuu niletee taarifa ya kila mkoa na wilaya kuna mapori mangapi tutakutana hapahapa kupeana mrejesho.”