Majaliwa asema hakuna kugawa maeneo mapya ya utawala
Muktasari:
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo Jumamosi Agosti 12 na Ofisi ya Waziri ilieleza kuwa Majaliwa alitoa kauli katika mkutano wa hadhara wa eneo Ulyankulu na Kaliua mkoani Tabora akiwa kwenye ziara yake ya kikazi.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imesitisha mchakato kutoa maeneo mapya ya utawala hadi itakapotangazwa vinginevyo.
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo Jumamosi Agosti 12 na Ofisi ya Waziri ilieleza kuwa Majaliwa alitoa kauli katika mkutano wa hadhara wa eneo Ulyankulu na Kaliua mkoani Tabora akiwa kwenye ziara yake ya kikazi.
"Tumesitisha mchakato wa kutoa maeneo mapya ya utawala ili tuimarishe kwanza yale ya awali. Tunaimarisha kwanza miundombinu ya majengo ya ofisi, nyumba za watumishi kwenye wilaya na halmashauri mpya na zikitengamaa tutafanya uamuzi upya," alisema Majaliwa katika taarifa hiyo.
Majaliwa ambaye pia ni Mbunge Ruangwa (Lindi) alieleza hayo wakati akijibu maombi ya wabunge wa majimbo ya Ulyankulu na Kaliua walisema kuna haja ya kuigawa wilaya ya Kaliua ili kusogeza huduma kwa wananchi waishio kwenye kata zilizo mbali na tarafa.