Lima nyanya kisasa-2

Muktasari:

Nyanya zinazoonyesha kuwa na sifa ya kuhifadhika bila kuharibika mapema ni kama:

Katika makala ya wiki iliyopita, nukta ya mwisho ilihusu aina za nyanya. Endelea.

Nyanya zinazoonyesha kuwa na sifa ya kuhifadhika bila kuharibika mapema ni kama:

(a)Tengeru’97 ambayo ina sifa zifuatazo: Huzaa sana kutokana na wingi wa matunda na muda mrefu wa kuvuna, ambao hufikia michumo mikubwa kati ya sita hadi saba.

Aina hii ina sifa ya kuwa na ganda gumu, hivyo haziharibiki haraka wakati wa kusafirisha au kuhifadhi (wastani wa siku 20). Zina sifa ya kuvumilia baadhi ya magonjwa kama vile ugonjwa wa kunyauka. Tengeru’97 hustahimili mashambulizi ya ugonjwa wa minyoo fundo (b) Tanya. Sifa kubwa ya Tanya ni kwamba nayo huzaa sana. Huwa na ganda/ngozi ngumu ambayo inazuia kuoza au kuharibika kwa urahisi wakati wa kusafirisha au wakati wa kuhifadhi kwa muda mrefu. Tanya nayo ina ladha nzuri inayopendelewa na walaji wengi.

Zingatia: Tatizo la Tanya na T97 ni kwamba si kubwa sana kama marglobe 2009. Lakini ukubwa ni karibu unge karibiana, haujapishana sana. Kwa ujumla, ukubwa na wingi wa mazao hutegemea sana matunzo, udongo, hali ya hewa na mazingira kwa jumla.

Maandalizi ya shamba la nyanya

Shamba la nyanya liandaliwe mwezi mmoja au miwili kabla ya kupanda miche. Mara baada ya kulima choma nyasi juu ya udongo au ondoa magugu yote yanayoweza kuhifadhi wadudu na magonjwa ya nyanya.

Siku moja au mbili kabla ya kuhamishia nyanya shambani, mwagilia sehemu iliyoandaliwa kwa ajili ya kuhamishia nyanya.

Andaa mashimo ya nyanya kutegemeana na idadi ya miche uliyonayo, nafasi na aina ya nyanya. Nafasi kati ya mche hadi mche ni wastani wa sentimita 50-60 na mistari ni 50-75 kutegemeana na aina au zao litakalo changanywa na nyanya.

Jinsi ya kupanda miche ya nyanya

Weka samadi viganja viwili au gram tano za mbolea ya kupandia kwenye shimo kabla ya kupanda mche. Hamisha miche toka kitaluni pamoja na udongo wake. Sambaza mizizi vizuri kwenye shimo bila kukunja.

Fukia miche kina kile kile ambacho shina lilikuwa limefukiwa kitaluni. Mwagilia maji ya kutosha kulingana na unyevunyevu uliopo kwenye udongo kisha weka matandazo na kivuli ili kupunguza uharibifu unaosababishwa na mionzi ya jua.

Umwagiliaji wa nyanya

Nyanya kama ilivyo kwa mazao mengine, zinahitaji maji mengi ili kuzaa matunda yenye afya. Kutegemeana na aina ya udongo, unaweza kumwagilia nyanya mara mbili kwa wiki.

Hakikisha unapanga ratiba maalum ya kumwagilia na unaifuata ili kuepuka kumwagilia kiholela holela kwani umwagiliaji usio na mpangilio huathiri afya ya matunda ya nyanya na kupelekea nyanya kuoza kitako. Unapotumia vifaa kama keni au mpira, jitahidi sana usimwagilie kwenye majani ya mmea au matunda kwa sababu kulowesha mmea kunavutia wadudu na magonjwa ya ukungu yanayoharibu nyanya.

Zingatia: usituamishe maji kwenye bustani au shamba la nyanya.

Palizi: Kudhibiti magugu

Hakikisha shamba ni safi wakati wote, palilia shamba na hakikisha magugu yote hasa yale ya jamii ya nyanya yamelimiwa chini. Palilia shamba lako wiki ya pili au ya tatu baada ya kupandikiza miche,. Lakini pia unaweza kupalilia kila unapoona magugu kwani shamba linatakiwa kuwa safi muda wote. Unaweza kuondoa magugu kwa kutumia dawa za kuua magugu au jembe la mkono.

Magugu ni hatari kwa sababu yanashindana na mimea katika kuchukua nafasi na hivyo mimea kushindwa kujitanua. Pili: magugu huzuia mimea ya nyanya kupata mwanga wa jua wakutosha hivyo kuifanya mimea kushindwa kujitengenea chakula cha kutosha.

Imeandaliwa na Mogriculture. 0655-570-084. www.mogriculture.com