Uhaba wa vifaranga wapaisha bei ya kuku Dar

Muktasari:

  • Baadhi ya viwanda vinavyototolesha havipokei tena maombi ya wateja huku madalali wa kampuni za mikoani nao wak-ipishana na fedha kwa kukosa bidhaa.

Kutokana na kuongezeka kwa hamasa ya ufugaji kuku, vifaranga wame-kuwa dili hivi sasa hasa jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya viwanda vinavyototolesha havipokei tena maombi ya wateja huku madalali wa kampuni za mikoani nao wak-ipishana na fedha kwa kukosa bidhaa.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kukosekana kwa bidhaa hiyo hivyo kuwakwamisha wafugaji wengi kuendeleza mradi huo kwa malengo wali-yojiwekea.

Hamimu Mlindwa ni miongoni mwa mael-fu ya wafugaji kuku ambao wameathiri-ka na hali hiyo baada ya kuhangaika kwa muda mrefu kutafuta vifaranga wanaowa-hitaji bila mafanikio.

“Kwa miaka miwili iyopita nilikuwa na kuku 1,000 wa mayai lakini wamezeeka na nikawauza. Sasa nilikuwa natafuta vifaranga 2,300 lakini havipatikani,” anasema.

Mfugaji huyu kutoka Kigamboni anase-ma licha ya kuandaa mabanda na chakula kwa ajili ya vifaranga hivyo, analazimika kuziangalia rasilimali zake ambazo hazi-tumiki kama alivyopanga.

Anasema amezunguka viwandani na kuwaona mawakala kadhaa wa vifaranga lakini kote huko ameambiwa hawezi kupa-ta kiasi hicho labda kuanzia mwishoni mwa Novemba.

UchunguziKuthibitisha malalamiko ya wafugaji wengi wanaopitia changamoto kama ya Mlindwa gazeti hili lilitembelea kiwan-da cha Interchick kilichopo jijini Dar es Salaam pamoja na mawakala wa vifaranga wanaopatikana Tazara kujiridhisha.

Pasi na shaka, Mwananchi limejiridhi-sha kuwapo kwa uhaba huo huku bei ya vifaranga wachache wanaopatikana ikipaa siku za hivi karibuni. Katika uchunguzi wake, mwandishi alitoa oda ya vifaranga 2,500 ambao hakuwapata.

Kutokana na viwanda vya jijini hapa kuelemewa na oda za wafugaji hulazimika kuagiza vifaranga kutoka Arusha na Moshi ili kukidhi mahitaji ya wateja.

“Tulikuwa tunategemea Interchick lakini nao hivi sasa wamezidiwa hivyo tunapoagiza vifaranga kutoka kampuni za mikoani, tukivipata hatuwezi kumpa mfan-yabiashara mmoja badala yake tunagawa kidogo kidogo kila mtu apate ili aendeleze ufugaji na wao wanaelewa kwa sababu hali halisi wanaiona,” anasema Nyamasana.

Kutokana na hali hiyo, anasema biashara imekuwa mbaya kwa wafugaji hata mawakala hao kwa kuwa mzunguko huwa mzuri.

“Bidhaa zinapokosekana mambo mengi hayaendi. Unakuta fedha unayo lakini huwezi kuizalisha jambo linalotuathiri kwa kiasi kikubwa,” anasema.

Uhaba huo umesababisha mabadiliko ya bei ya vifaranga wa kuku na mayai na nyama pia. Hivi sasa kifaranga kimoja cha nyama kinauzwa Sh2,300 kutoka Sh1,600 huku wale wa mayai wakiuzwa kati ya Sh2,800 hadi Sh3,000 kutoka Sh2,300 miezi michache iliyopita.

Wakala wa vifaranga katika eneo la Tazara, Paschal Nyamasana anasema licha ya bei kuongezeka bado uhitaji ni mkubwa kutokana na uzalishaji wa ndani kushindwa kukidhi mahitaji ya wafugaji waliopo.

“Watu wengi hivi sasa wanaingia katika ufugaji jambo linawaelemea wazalishaji na uhaba huu umekuwa ukiwarudisha nyuma wafugaji kiasi cha baadhi kuanza kukata tamaa kutokana na kusubiri kwa muda mrefu,” anasema Nyamasana.

Wakala mwingine wa vifaranga, Soviet Manda anasema kutokana na ugumu wa upatikanaji wa bidhaa hiyo hivi sasa mteja anatakiwa kuweka oda na kusubiri kuanzia wiki tatu.

“Kwa vifaranga 2,500 sasa hivi ni ngumu kuvipata kwa pamoja labda usubiri lakini utapata awamu. Baada ya wiki tatu utapewe vifaranga 1,000 katika awamu ya kwanza, kisha 1,000 wengine na mwisho utapewa 500 waliopbaki,” anasema Manda alipoulizwa kama kuna uwezekano wa kupata vifaranga 2,500 kwa wakati mmoja.

Anasema vifaranga wengi anaouza hivi sasa huwatoa Arusha ingawa zamani alikuwa anawapata kutoka Kenyapia. Kwa hali ilivyo anaiomba Serikali kuangalia athari zitokanazo na marufuku ya kutoingiza vifaranga kutoka nje.

Hali ikiwa hivyo kwa mawakala hao, katika kampuni ya Interchick Mwananchi liliambiwa linaweza kupata kiasi chochote cha vifaranga wa nyama kuanzia Desemba huku oda ya vifaranga wa nyama ikiwa imefungwa.

“Hatupokei oda ya vifaranga wa nyama kabla ya hizi zilizopo hazijakwisha na hatujui tutazimaliza lini,” alisema muhudumu aliyekutwa kiwandani hapo.

Marufuku

Wote; wafugaji na mawakala wanailalamikia Serikali kuona umuhimu wa kuondoa zuio la kuingiza vifaranga kutoka nje ya nchi.

Oktoba mwaka jana, Serikali iliteketeza vifaranga 6,400 waliokuwa wanaingizwa nchini kwa njia za panya kutoka nchini Kenya ikiwa ni utekelezaji wa zuio la kuingiza kuku za mazao yake.

Uchomaji wa vifaranga hivyo ulifanyika Namanga ukisimamiwa na maofisa wa Mamlaka ya Dawa na Chakula (TFDA), Wizara ya Mifugo, Mamlaka ya Mapato (TRA) na vyombo vya usalama.

“Tumevichoma ili visisambazwe tena nchini kwa kuwa hatujui usalama wake hasa kutokana na kuwapo kwa taarifa za ugonjwa wa mafua ya ndege nchi jirani,” alisema ofisa mfawidhi wa Kituo cha Udhibiti wa Magonjwa ya Mifugo Kanda ya Kaskazini, Obedi Nyasebwa.

Nyasebwa alisema wameteketeza vifaranga hivyo kwa kuzingatia Sheria ya Magonjwa ya Wanyama namba 17 ya mwaka 2003 na tangazo la mwaka 2007 la kupiga marufuku kuingizwa nchini vifaranga vya kuku na mayai.

Mapema mwaka jana, naibu waziri wa iliyokuwa Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, William Ole Nasha alisema Serikali imeteketeza vifaranga 67,500 kutoka nje ya nchi vilivyoingizwa nchini kinyume cha sheria kati ya mwaka 2013 hadi 2017.

Nasha alikuwa anajibu swali lililoulizwa na aliyekuwa Mbunge wa Ukonga (Chadema), Mwita Waitara aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani wa kuzuia uingizaji mayai kutoka nje kwa sababu yanaharibu soko la ndani.

Naibu waziri huyo alisema hakuna mwekezaji yeyote aliyepewa kibali cha kuingiza vifaranga au mayai nchini tangu Serikali ilipozuia suala hilo tangu mwaka 2006 ili kudhibiti ugonjwa wa mafua ya ndege kuenea na kuwasababishia hasara wafugaji.

“Sheria ya Magonjwa ya Wanyama namba 17 ya mwaka 2003 na kanuni zake za mwaka 2007 na 2010 zinatumika kudhibiti na kukagua uingizaji maeneo ya mpakani, bandarini na viwanja vya ndege,” alisema.

Kwa kutambua msimamo wa Serikali, Mlindwa anasema viongozi hawajui madhira wanayopitia wafugaji kutokana na zuio hilo.

“Nimeandaa chakula na kuongeza mabanda ili niingize vifaranga wengi zaidi ya niliokuwa nao awali lakini hawapatikani. Ningeweza kuagiza kutoka nje lakini Serikali imezuia hivyo nakaa na fedha zangu mkononi huku mikikiangalia chakula nilichoandaa kwa ajili ya vifaranga,” anasema mfugaji huyo mdogo.

Kukosekana kwa vifaranga kunawagusa wachomaji wa kuku pia. John Michael wa wa Mtoni Kijichi anasema upatikanaji umekuwa mgumu na bei imepanda. Zamani anasema walikuwa wananunua kwa kati ya Sh4,500 hadi Sh5,000 lakini sasa hivi ni Sh5,500 hadi Sh6,500.

“Tunauza kwa sababu ni biashara tuliyoizoea na hatuna kazi nyingine. Hatujapandisha bei kwa sababu wateja hawana pesa na tukiongeza tunaweza kuwapoteza,” anasema.

Muuzaji wa chipsi eneo la Ubungo Riverside, Mahanja Kimaryo anasema awali alikuwa anachukua kuku kwa oda lakini sasa analazimika kutafuta sehemu tofauti.

“Kila siku huwa nachukua kuku 60 ambao nilikuwa nakuta wameandaliwa kabisa lakini sasa hivi idadi hiyo huwa haifiki jambo ambalo linanilazimu kutafuta sehemu nyingine,” anasema Kimaryo.

Serikali

Kaimu mkurugenzi wa huduma za mifugo wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Martin Ruheta anasema zuio la kutoingiza kuku wala bidhaa zake kutoka nje ni mkakati wa kukabiliana na mafua ya ndege ambayo yamesambaa katika nchi duniani.

“Serikali inafahamu juu ya uhaba wa vifaranga uliopo. Tumetoa kibali kwa kampuni ya Interchick kuagiza mayai ya kutotoreshea,” alisema Dk Ruheta.

Hata hivyo, anasema uhaba uliopo utapata suluhu ya kudumu baada ya wawekezaji wanaojenga kiwanda cha kutotoresha vifaranga watakapoanza uzalishaji hapo Oktoba.

Ufugaji wa kuku nchini umetawaliwa zaidi na kuku wa kienyeji ambao huunda asilimia 90. Licha ya changamoto za magonjwa na uzalishaji mdogo uliopo, ni kitoweo muhimu zaidi vijijini.

Asilimia 10 inayobaki ni kuku wa kisasa ambao hufugwa zaidi mjini kwa mfumo wa biashara. Mpaka Oktoba 2015, takwimu za Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) zinaonyesha kulikuwa na jumla ya kuku milioni 39.5 nchini. Kati yao; zaidi ya milioni 37 walikuwa wa kienyeji, milioni 1.57 wa mayai na 885,584 wa nyama.