Zijue mbinu kumi na mbili za kuzalisha mayai mengi kwa mfugaji

Muktasari:

  • Imekuwa kawaida kusikia mtu amejiajiri mwenyewe kupitia ufugaji wa kuku. Fursa nyingi za soko la kuku na mazao yake sambamba na elimu elekezi zinazotolewa mara kwa mara kwenye makongamano, warsha, semina na vyombo vya habari kama makala haya.

Tunaendelea kuibua na kuonyesha njia nyingi za kufanikiwa katika ufugaji wa kuku ambao ndiyo ndoto kubwa kwa wafugaji wengi. Fursa ya ufugaji inazidi kuchanua na kufanya vizuri kila kukicha kutokana na teknoloji kushamili.

Imekuwa kawaida kusikia mtu amejiajiri mwenyewe kupitia ufugaji wa kuku. Fursa nyingi za soko la kuku na mazao yake sambamba na elimu elekezi zinazotolewa mara kwa mara kwenye makongamano, warsha, semina na vyombo vya habari kama makala haya.

Mwendelezo huu wa uchambuzi wa leo unajikita katika kanuni bora za uboreshaji wa miradi yote ya kuku. Karibu upate kujuzwa mbinu 12 za kuzalisha mayai mengi shambani kwako.

Kwa wale wasiopata makala haya kwa mwendelezo napenda kuwapa vidokezo vilivyopita kujadililiwa kwenye makala yaliyopita na kuwakumbusha kuwa makala haya hutolewa kila jumamosi.

Na hivi karibuni tulijadili juu ya sababu za kuku kunyonyoka manyoya, kukinga magonjwa hatarishi na sababu 10 za kukosa mayai kwa kuku. Leo ni mbinu 12 za kuzalisha mayai mengi kwa mfugaji.

Mbinu ya kwanza ni Kuchagua mbegu ya kuku. Aina au mbegu ya kuku ndiyo siraha ya kwanza katika mbinu za kuzalisha mayai mengi shambani. Sio kila kuku anataga mayai mengi.

Zipo mbegu za kuku wanaotaga sana na nyingine zisizo taga mayai mengi. Ukiwa mfugaji mwenye lengo la kuzalisha mayai mengi kitu cha kwanza ni kupata mbegu ya kuku wenye asili ya kuzalisha mayai mengi.

Hata mkulima wa mazao shambani huchagua mbegu inayozaa sana shambani kwake. Hivyo chagua mbegu ya kuku inayotaga sana kama lengo lako ni kupata mayai mengi.

Mbinu ya pili ni kuzuia vifo vya kuku shambani. Kimsingi sio rahisi kuzuia vifo kwa sababu vifo ni sehemu ya maisha. Lakini vifo vingi hutokana na sababu zenye kuweza kuzuilika.

Zuia vifo kwa nguvu zote kwa kuziba mianya ya vifo kama vile kuimarisha kinga na tiba kwa magonjwa ya mlipuko, kuliwa na wanyama, kukosa hewa, joto kali na lishe. Vifo vikizidi kiwango huathili uzalishaji wa mayai na mavuno kwa mfugaji.

Mbinu ya tatu ni kuzingatia umri wa kuku. Kawaida kuku wa mayai wenye asili ya kuzalisha mayai mengi huanza kutaga wakiwa na umri wa wiki 20 na kuendelea hadi wiki 70 sawa na mwaka mmoja tangu kuanza kutaga kwao. Kipindi hiki cha utagaji ni kizuri kwa mfugaji kuvuna mayai.

Zaidi ya hapo mayai yatashuka kiasi cha kukosa faida. Hivyo uzalishaji uwe ndani na kipindi hiki kisha uza kuku wote na kuingiza wengine wapya. Ni vizuri kuingiza vifaranga watakaorithi mapema walau miezi sita kabla ya kuwauza wanaozalisha kwa wakati huo ili unapouza kuku wazee kuku wapya wawe tayari wameanza kutaga.

Mbinu ya nne ni kudhibiti uzito wa kuku. Wastani wa uzito wa kuku wenye kutaga sana ni kilo 1.5 zaidi au pungufu mno ya uzito huu kuku hatagi vizuri. Udhibiti huu wa uzito ufanyike katika ulishaji wa chakula. Mfugaji anashauriwa kulisha chakula kwa kipimo ili wasinenepe kuzidi kiasi au kuwapunja chakula chini ya kiasi wanachotakiwa kula wakakonda. Jambo la kuzingatia katika kudhibiti uzito ni kiasi na ubora wa chakula, chakula duni kuku watapungua uzito hata kama wanapewa kingi.

Mbinu ya tano ni kutengeneza banda rafiki kwa maisha ya kuku na mfugaji mwenyewe. Kwa kawaida kuku wanamahitaji yanayojulikana kama vile nafasi ya kutosha, hewa safi na joto la wastani bandani.

Ubunifu na uboreshaji zaidi wa mambo haya mfugaji anaweza kuongeza uzalishaji wa mayai. Kwa mfano mbinu ya kuweka kuku wengi kwenye chumba kidogo ni moja kati ya ubunifu.

Badala ya kufugia sakafuni mfugaji anaweza kuweka cages na kufuga kwa njia ya vizimba kuku wengi wakaingia kwenye chumba.

Mbinu ya sita ni kuondoa kuku wasiotaga. Katika kundi la kuku wengi, kuku wasiotaga hawakosi. Mfugaji anaweza kuchambua kuku wanaotaga na wasiotaga vizuri na kuwatenga.

Wasiotaga kabisa na wanaotaga kidogo anaweza kuwauza kuwauza kupunguza gharama ya chakula. Kwa mfano kuku wagonjwa bila dalili ya kupona, kuku walio wadogo sana kuliko kawaida kwenye kundi au kuku wasiohusika kama vila majogoo kwenye mitetea wanaotaga mayai ya kuuza bila kuangulisha au kuku wa kienye kwenye kundi la kuku wa mayai wa kisasa wote hao ni kuku wa kuchambuliwa na kuuzwa.

Kwa upande mwingine mfugaji anatakiwa kuwa mwangalifu anapotaka kufanya jambo lingine baada ya kukamilisha jambo la kwanza. Mara nyingi kila kitu unachotaka kufanya kinahitaji maandalizi na uchunguzi wa kujilithisha.

Pia mbinu hizi za kuzalisha mayai mengi kwa kuku hutegemeana hivyo inatakiwa kila mbinu kuifanyia mazoezi ya kutosha kiasi cha kuifanya vizuri. Au unaweza kujifunza kwa waliofanya mbinu hiyo mara kwa mara wakajua ufanisi wake.

Usijifunze kwa mtu aliyefanya kulipua ni rahisi kukukatisha tama na kukupoteza. Pata maelezo kwa wataalamu wenye kuaminika unapohitaji msaada wa maelekezo kufanya mbinu moja wapo kati ya mbinu hizo hapo juu utafauru vizuri.

Mbinu zingine sita juu ya kuzalisha mayai mengi zitakujia kwenye makala yajayo kukamilisha mbinu kumi na mbili.