Kama mchezaji hukupapatikiwa, hebu jitathimini

Muktasari:

  • Simba ambayo imezawadia wachezaji wake kwa kazi nzuri, imeifanya kazi barabara kwa kutengeneza kikosi makini kwa ajili ya msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara. Hata hivyo, hiyo si ishu sana, hapa nina majambo mawili ninayotaka kuyazungumza; Azam FC na wachezaji kujitathmini.

Ligi Kuu Tanzania Bara imemalizika kwa timu ya Simba kutwaa ubingwa iliokuwa ikusaka kwa miaka mitano ndani ya misimu mine.

Simba ambayo imezawadia wachezaji wake kwa kazi nzuri, imeifanya kazi barabara kwa kutengeneza kikosi makini kwa ajili ya msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara. Hata hivyo, hiyo si ishu sana, hapa nina majambo mawili ninayotaka kuyazungumza; Azam FC na wachezaji kujitathmini.

Nikianza na Azam. Imemaliza Ligi Kuu ikiwa nafasi ya pili na sababu kubwa ni baada ya kuboronga katika mechi zake na wakati mwingine mechi ambazo hata hazistahili kupoteza.

Inawezekana mtu akanishangaa kuwa haistahili kufungwa, kivipi wakati soka ina hali tatu. Sawa. Nikiangalia timu hii na timu nyingine za Ligi Kuu unaweza kusema ni sawa tu.

Maana yangu ni kwamba, nilitarajia kuiona Azam ikitikisa miamba ya soka Tanzania, Azam ilikuwa iwe timu moja kali na tishio hata Afrika Mashariki na Kati.

Wachezaji wa Azam wamebweteka, hawachezi kazi kazi, hawajitumia inavyotakikana ile ya kufia uwanjani kwa kuwa hawana wasiwasi na posho na mishahara inaingia. Hapa ni Kipre tu.

Hii ni mbaya. Matokeo yake gharama zinakuwa kubwa wakati timu haipafomu. Kuna kufungwa, lakini ilivyo Azam si ya kufungwa na Mwadui au kutoka sare na Ruvu Shooting, ilitakiwa hapo ni kukandamiza tu.

Maana yangu ni nini, Azam wana gym, bwawa la kuogelea, uwanja wa mazoezi na saa yoyote unajifua lakini angalia matokeo ya timu. Mfano, wachukue Mbeya City wageuze Azam na Azam wawe Mbeya City, huo mpira ninaamini watu watatafutana. Wachezaji wa Azam wameshakuwa mamwinyi.

Tuyaache. Baada ya ligi Kuu kumalizika, timu zinapambana kufanya usajili.

Kwa wachezaji sasa, inatakiwa mchezaji kujitathmini, kujiuliza, kwanini hupapatikiwi na mchezaji mwenzako anapapatikiwa? Umecheza naye timu moja, kwanini mwenzako analetewa mabulungutu ya noti wewe huletewi, mwenzako anagombewa wewe kwanini hugombewi?

Hiyo ni kwa sababu ana kitu cha ziada ameonyesha. Ukijiangalia utajiona kuwa wewe ni mvivu, hujitumi, huna vitu vya ziada na ndiyo maana huonwi, huonekani!

Ni ngumu sana kuwa na kitu cha ziada, kujituma, kucheza jihad na kisha usionekane.

Ndiyo maana nikasema wachezaji wajitathimini, waangalie wamekosea wapi na kuongeza bidii msimu ujao. Mimi naona wachezaji wanazikataa fedha wenyewe, wachezaji hawataki mabulungutu ya usajili, kama kweli unataka mamilioni, kwanini usijitume, kwanini usifanye vitu vya ziada. Cheza uonekane.

Mchezaji anaingia mazoezini amechelewa, kwa wanaoachiwa hawajichungi, hawazingatii muda wa kulala, chakula, miiko ya uchezaji na wenyewe ni kuendekeza starehe, matokeo yake wanachemka.

Hii ni changamoto kwao kwa msimu ujao. Kwanza kumshawishi kucheza kwa kujituma mazoezini, kuwa wabunifu uwanjani.

Inachotakiwa ni mchezaji kufanya mazoezi ya ziada na uzuri wachezaji watakuwa na ‘fatigue’ au kuumia kwa wale wa mara kwa mara kwa kuwa mechi ni nyingi, hivyo ni wakati wa kuonyesha uwezo.

Mchezaji lazima uangalie mwenzako ana kipi cha ziada? Kakuzidi nini akagombewa? Jiangalie, ukiona hivyo ujue una walakini.