Ronaldo aendelea kutikisa Real Madrid

Kiungo wa Real Madrid, Marco Asensio (kushoto) akiwania mpira na beki wa Atletico Madrid, Jose Gimenez wakati wa mechi ya ‘Madrid Derby’ juzi kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu. Picha ya AFP

Muktasari:

  • Ubutu wa safu ya ushambuliaji ya Real Madrid  inayoongozwa na Gareth Bale  imewafanya  mashabiki wa  klabu hiyo  kumkumbuka starika wao Cristiano Ronado aliyejiunga hivi karibuni na  Juventus.
  • Suluhu  dhidi ya wapinzani wao kutoka mji mmoja Athletico Madrid Jumamosi iliyopita iliwainua vitini mashabiki wa Real Madrid na kuanza kuimba "Ronaldo" "Ronaldo".
  • Kushindwa kushinda katika mechi mbili mfululizo  kumewatia hasira mashabiki wa Real Madrid ambao wanaamini kama wangepata ushindi wangekwea kileleni  kwenye msimamo wa ligi.

Inawezekana mashabiki wa Real Madrid hawajakubali kabisa kuondoka kwa straika wao matata, Cristiano Ronaldo.

Mara zote mambo yanapokuwa magumu, humkumbuka kwa kuwa alikuwa mtu wa kuamua matokeo. Real Madrid kwa sasa haina huyu mtu.

Pale mbele kwa sasa yupo Gareth Bale lakini hajafikia mavitu ya Ronaldo. Hata akiwa pamoja na Karim Benzema lakini mambo bado.

Unaambiwa katika mchezo wa juzi wa ‘Madrid Derby’ kati ya Athetico Madrid na Real Madrid, hakukuwa na mbabe kwani baada ya dakika 90, matokeo yalikuwa 0-0.

Lakini mashabiki walimkumbuka sana Cristiano Ronaldo, walikuwa wakiimba “Ronaldo, Ronaldo” ambaye hayuko tena kwenye klabu hiyo baada ya kutua kikosini Juventus dirisha lililopita.

Kelele za Ronaldo ni baada ya Real Madrid kushindwa kushinda mechi mbili mfululizo ambazo kama ingefanya hivyo, ingeupeleka kileleni mwa La Liga. Suluhu ya Atletico Madrid ndiyo iliyowatia hasira.

Real, ilifungwa na Sevilla katikati ya wiki, na ingeweza kuiengua kileleni Barcelona, ambayo nayo ilitoka sare na Athletic Bilbao mapema kabisa.

Straika Gareth Bale aliyekuwa akitarajia kucheka na nyavu, alilazimika kutoka baada ya kuumia.

Atletico ilikosa nafasi na yenyewe baada ya Antoine Griezmann, kutandika shuti kali lililodakwa na Thibaut Courtois.

Diego Costa alipambana kupata bao lakini alishindwa kufunga ikiwa ni mechi yake ya 16 bila bao.

Mabingwa hao wa Ulaya watakuwa na kazi kesho dhidi ya CSKA Moscow wakati Atletico ambao ni mabingwa wa Europa, wataialika Club Brugge siku itakayofuata.