Ukoloni Mamboleo na namna viongozi Afrika walivyonaswa

Muktasari:

  • Ikumbukwe kwamba tangu karne ya 15 hadi karne ya 19 bara la Afrika lilikuwa sehemu muhimu pengine kuliko sehemu yoyote duniani kwa sababu ndilo lilikuwa mzalishaji mkuu wa malighafi kwa ajili ya mataifa ya Ulaya.

Mwaka 1884-1885 ulifanyika mkutano wa mataifa ya Ulaya nchini Ujerumani kuhusu namna ya kuligawana bara Afrika. Mkutano huo ulisimamiwa na aliyekuwa Kansela wa Ujerumani kwa wakati huo, Otto Bismark na kufikia makubaliano ya kila nchi inayoweza kutawala sehemu yoyote ya Afrika na rasilimali zake, ichukue.

Ikumbukwe kwamba tangu karne ya 15 hadi karne ya 19 bara la Afrika lilikuwa sehemu muhimu pengine kuliko sehemu yoyote duniani kwa sababu ndilo lilikuwa mzalishaji mkuu wa malighafi kwa ajili ya mataifa ya Ulaya.

Historia inatuambia kwamba mataifa ya Denmark, Ufaransa, Urusi, Ureno, Italia, Hispania, Uturuki, Uholanzi yaligawiwa maeneo huku Ubelgiji na Marekani wakiwa kama wageni waalikwa.

Kweli mkutano huo ulileta mafanikio katika kile walichokidhamiria ikiwa ni pamoja na kuepusha migongano kati yao, kwani kila taifa lilikuwa na uchu wa rasilimali za bara hili.

Masuala yaliyoafikiwa katika mkutano huo yalikuwa ni kukomesha biashara ya utumwa, kueneza kile walichokiita ustaarabu na dini na kukomesha vita vya wenyewe vya wenyewe vilivyopiganwa na makabila na koo mbalimbali zilizokuwapo wakati huo. Hata hivyo, masuala haya hayakuwa mambo ya msingi sana kwao.

Hapo awali niligusia kwamba Afrika ilikuwa sehemu muhimu sana duniani kwa kuwa ilikuwa mahala pekee ambapo wangeweza kupata malighafi kwa ajili ya viwanda huko Ulaya na Marekani. Kila nchi wakati huo ilitamani kumiliki ardhi ya Afrika yenye rutuba, madini na kila nchi ilitamani iwatumie Waafrika kama nguvukazi katika mashamba yao. Kupitia mtifuano huo ndipo Bismarck akawaita wenzake mjini Berlin. Hapa ndipo historia inapotuambia kwamba Afrika ikakatwa vipandevipande, wakaingia kama mtu aliyeingia kwenye shamba ambalo alipanda yeye na kuvuma mazao yake. Wakakubaliana kwamba kila nchi miongoni mwao inaweza kuchukua koloni lolote kwa sharti tu la kuweza kutawala, hakuna taifa la Ulaya ambalo lingezuiwa kwa namna yoyote kufanya biashara katika bara la Afrika, hapakutakiwa kuwa na ongezeko la kodi kwa bidhaa yoyote kutoka au kuingia Afrika.

Vitabu vinaniambia madini yote na misitu minene ya mbao na magogo ya Kongo akapewa Mfalme Leopold II wa Ubelgiji, Uingereza ikachukua shaba ya Zambia, mafuta na ardhi yenye rutuba ya Nile huko Misri, Kenya, Sudan na dhahabu ya Kimberley, Afrika Kusini, Ghana na almasi ya Zimbabwe. Ufaransa ikapewa kila kitu kilichopatikana Jamhuri ya Afrika ya kati, Mauritania mpaka Gabon na Chad. Ureno akaambiwa ajichukulie Msumbiji na Angola. Italia ilichukua Somalia na sehemu za Ethiopia. Bahari, madini, mbuga za wanyama na ardhi nzuri ya Tanzania bara (Tanganyika kwa wakati huo) na Namibia alijichukulia Mjerumani.

Katika hayo yote Mwafrika hakuhusishwa, alikuwa hana hili wala lile mpaka alipokuja kujua kwamba yeye anapaswa kulima na kuchimba madini yake mwenyewe kisha awape hawa watu wapeleke kwao kisha watulete sigara, vioo, mafuta na nguo watuuzie, inauma sana.

Kwanini nimeanzia huko?

Huku ikiwa imepita miaka zaidi ya 50 tangu mataifa haya yaiache Afrika kwa kila kinachoitwa uhuru, mataifa haya yanaonekana kurudi tena kwa kasi katika miaka ya hivi karibuni. Wakuu wa mataifa yaleyale yalikaa mwaka 1884-1885 yameanza kupishana kwa kasi ya ajabu katika anga la bara la Afrika. Wanakuja kwa njia ya makubaliano na mikataba ya kiuwekezaji.

Mifano ya hivi karibuni kabisa ni ujio wa waziri mkuu wa Uingereza, Kansela wa Ujerumani, marais wa China (Hu Jintao na Xi Jinping). Sambamba na hili kukawa na mkutano wa China na viongozi wa Afrika wa uliofanyika China, huko tuliahidiwa dola 60 bilioni.

China inaitaka Afrika huku ikifanikiwa kwa kiasi kikubwa Afrika ya Mashariki; Uingereza inakomaa na Kenya, Afrika Kusini na Nigeria na Ujerumani ikakomaa na Senegal, Ghana na Nigeria huku Ufaransa kupitia mkutano uliofanyika Mei mwaka huu mjini Paris, ikitangaza dhamira ya kuisaidia Afrika zaidi ya Euro 65 milioni.

Si hao tu, hata marais waliopita wa Marekani (Obama na Bush) wamefanya ziara Afrika, ikiwamo nchini mwetu na kuzungumzia mipango mbalimbali.

Tujiulize, kwa nini?

Katika makosa ambayo Afrika haipaswi kuyarudia ni kuacha mataifa haya yajichagulie cha kuchukua. Kwa sasa mataifa haya yanajua Afrika ina wasomi, wanaelewa wazi kwamba sasa hivi Afrika ina watu wenye uwezo wa kuchakata mambo, hivyo wanapaswa kutulia na kuja na mikakati inayoonekana kama pipi kumbe ndani shubiri.

Kwa sasa mataifa haya hayawezi kutumia mbinu waliyoitumia mwaka 1884-1885 au nyingine walizozitumia huko nyuma. Ni wakati wa kuwa makini.

Tusizubaishwe na mikopo yao ambayo huja kama neema kwa Afrika. Fikiri kuhusu Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na Benki ya Dunia na mashirika mengine namna yanavyoinyemelea Afrika baada ya kushindwa kurejesha madeni. Suala la mikopo halijaanza leo, suala la mahusiano ya kibiashara hayajaanza leo, yalikuwepo tangu miaka ya 1,700 walipotudanganya kwa vioo, sigara, bunduki na nguo, kisha wakachukua rasilimali ambazo mpaka leo hazijulikani thamani yake kwa sababu nyingine hazipimiki.

Kwa sasa Afrika ina viongozi na wataalamu wenye ufahamu wa kutosha kabisa kugundua mitego na hila iliyoko katika mikataba yao. Kumbuka haya mataifa yanataka Afrika iendelee kuyategemea ili yenyewe yaendelee kunawiri, kwa hiyo yale yote yanayosemwa kwamba yanatoka kwao kutusaidia yachunguzwe mara nyingi iwezekanavyo. Kuna haja ya kuwa makini sana na hawa watu.

Hebu tuwatumie wataalamu tulionao hata kama ni wa kiwango kidogo lakini kwa manufaa yetu. Mataifa ya Kiafrika yanapaswa kuwaamini wasomi wake wa masuala mbalimbali kwa sababu hata wataalamu tunaowaamini kutoka mataifa ya nje ya Afrika walianza kama sisi tu, hawakuzaliwa wanaweza, walijifunza.

Afrika kwa sasa ina wataalamu karibu kila idara, watumike watatusaidia. Sisemi kwamba tusishirikiane wala kuwatumia wataalamu kutoka nje, tushirikiane nao huku tukiwekeza nguvu kubwa kwa hawa wetu, tufanye hivyo, lakini kwa umakini mkubwa kuliko umakini ambao tumewahi kuwa nao siku za nyuma.

Afrika isitegemee misaada

Hivi inakuaje bara kama Afrika lenye kila kitu tena kwa kiwango cha kutisha bado linaishi kwa kutegemea misaada? Ni ajabu lakini ni kweli kwamba Afrika inategemea misaada kutoka kwa watu ambao wanatutegemea sisi kupata wanachotuletea.

Ifike mahala tutambue na tuamini kuwa haya mataifa hayawezi kufanya chochote bila Afrika, yaani tuume meno na tukamate breki hata kama tutaumia lakini baadaye watatuheshimu.

Kuishi kwa kutegemea misaada kwa watu ambao wanatutegemea sisi kupata wanachotuletea ni kichekesho kinachoweza kumfanya mtu acheke karne nyingi, niamini mimi kwamba hata wao wanatung’ong’a. Tusiwe waoga, kuna baadhi ya mambo ambayo tunaambiwa tuyatekeleze ndipo tusaidiwe, lakini ukiangalia nyuma yake kuna madhara makubwa. Hata hivyo, baadhi ya viongozi wa Afrika hukubali tu kusaini ili tupate misaada, lakini baadaye tunaingia kwenye mtego unaotulazimu kufia ndani.

Mfano, mataifa mengi yamekuwa yalikubali kuingia kwenye madeni ambayo yanakuwa matamu kwa nje, yaani kikitajwa kiasi cha hilo deni wanafikiri watanufaika lakini baadaye tunashindwa kulipa.

Tuziamini bidhaa za kiafrika pamoja na kuboresha uzalishaji wake. Ni ukweli usiopingika kwamba kuna baadhi ya sekta hasa kilimo bado zipo chini. Ukija sokoni unakuta bei ni ndogo, muda mwingine wakulima wanalanguliwa bidhaa zao.

Kutokana na hili unakuta uzalishaji unapungua, uzalishaji ukipungua maana yake tunajikuta tukitegemea bidhaa za vyakula kutoka nje. Sio hivyo tu, hata vile viwanda vilivyopo katika nchi za Afrika vinakufa kwa sababu bidhaa zake hazinunuliwi kwa sababu ya Waafrika hususani Watanzania kutokuviamini vya kwetu. Tujifunze kutumia vya nyumbani, licha ya kuamini kuwa vya nje vina ubora, vipo vingi pia vina ubora.

Serikali za kiafrika ziimarishe mifumo ya elimu. Kila kitu kinachofanyika kwa ufanisi katika ulimwengu huu kinategemea elimu. Ikiwa bidhaa zitakosa ubora, majengo yatakosa uimara, barabara hazitadumu, utawala utayumba, sekta za kilimo zitayumba, sekta ya fedha itayumba, sekta ya afya itayumba usiende mbali, chunguza elimu inayotolewa Afrika.

Elimu ikiwa mbovu hatuwezi kupata wataalamu wazuri wa masuala mbalimbali jambo ambalo litatufanya tuendelee kutegemea wataalamu wa afya, uchumi, wahandisi, wataalamu wa viwanda na madini ambao wakija wanaambatana na masharti kutoka nchi husika.

Elimu ikiwa mbovu mikataba mibovu hatuwezi kuikwepa, tutasaini tu kwa sababu hatuelewi. Zamani walituchukua, safari hii tusijipeleke wenyewe.

Mwandishi ni mwanafunzi wa Shahada ya kwanza ya Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Anafanya mazoezi kwa vitendo Mwananchi Communications Ltd na anapatikana kwa namba 0672395558