Makamba abadili wakurugenzi wakuu NEMC

Muktasari:

Miongoni mwa matatizo aliyoyabaini Waziri Makamba ni pamoja na kuwapo mazingira ya rushwa katika kutengeneza vyeti, urasimu na kuwatisha wateja ili watoe chochote.

Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Januari Makamba amefanya mabadiliko makubwa kwenye Baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC).

Akizungumza leo Jumatatu, Julai 17, Makamba amesema amebaini mazingira ya rushwa katika kutengeneza vyeti ambavyo havijafuata mchakato stahiki na urasimu.

Mengine ni kutokuwa na lugha nzuri kwa wateja na kuwatisha ili watoe chochote na kuzitumia kampuni binafsi za watumishi wa NEMC kufanya kazi za ukaguzi/uhakiki wa ndani ya NEMC kwa kisingizio cha kutokuwa na watumishi wa kutosha.

Pia amewasimamisha kazi  Manchare Heche, Deus Katwale, Andrew Kalua na  Benjamin Dotto  huku wengine wakiendelea kuchunguzwa wakati wizara ikiendelea kupokea taarifa za ziada.

 

Pia Waziri amefanya mabadiliko ya wakuu wa kanda;

*Jafari Chimgege, aliyekuwa Kanda ya Mashariki, sasa atakuwa Mkuu wa Kanda ya Dodoma.

*Goodlove Mwamsojo, aliyekuwa Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu-Mbeya, sasa atakuwa Mkuu wa Kanda ya Mashariki-Dar es Salaam.

*Dk Ruth Rugwisha, aliyekuwa Mkuu wa Kurugenzi ya Sheria, sasa atakuwa Mkuu wa Kanda ya Ziwa Mwanza;

*Dk Vedastus Makota, aliyekuwa Mkurugenzi wa

Mawasiliano, sasa atakuwa Mkuu wa Kanda ya Kusini - Mtwara;

*Joseph Kombe, aliyekuwa Mkuu wa Kurugenzi ya Utafiti na Mipango anakwenda kuwa Mkuu wa Kanda ya Kaskazini-Arusha.

*Dk Menard Jangu aliyekuwa Kanda ya Arusha anarudishwa Makao Makuu ya NEMC kuwa Kaimu Mkuu wa Kurugenzi ya Utafiti na Mipango.

*Jamal Baruti, aliyekuwa Mkuu wa Kanda ya Ziwa, anarudi Makao Makuu NEMC.

*Lewis Nzari aliyekuwa Mkuu wa Kanda ya Kusini –

Mtwara, sasa anakuwa Mkuu wa Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.