Makonda ammwagia sifa Meya Mwita kwa mara nyingine

Muktasari:

Amesema kundi la mameya wanaoendelea kumtukana rais, litaishia kuhesabu matusi tu na mwisho wake sheria itachukua mkondo wake.


Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amemmwagia sifa Meya wa Jiji hilo, Isaya Mwita akisema ni kiongozi atakayeendelea kung’aa katika uongozi wake kutokana na kazi anazofanya kwa ajili ya Watanzania.

Makonda ametoa kauli hiyo leo Machi 17, 2018 wakati wa mkutano wa kuzindua utalii wa ndani katika mkoa huo, akisema meya wa aina hiyo ni lazima kupata ushirikiano wa ofisi yake tofauti na mameya wanaobakia kumtukana rais.

Katika mkutano huo, RC Makonda amesema Mwita ni mwanasiasa mwenye dhamira njema ya kuwatumikia Watanzania, kama ilivyo kwa dhamira ya rais John Magufuli.

“Pia niendelee kukupongeza Meya wa jiji la Dar es Salaam, kaka yangu na ndugu yangu, na timu yako ya madiwani kwa kazi kubwa unayoifanya, katika jiji tunao madiwani wa vyama vyote ila meya wetu wa jiji ni wa tofauti, ni meya anayetazama maendeleo, anayetaka kazi, tangu nifahamiane naye kila anapokuja ofisini kwangu, ni mpango wa namna gani tunafanya kazi, ndiyo maana ataendelea ‘ku-shine’ kuliko mameya wengine wa upinzani,”amesema.

Amesema kundi la mameya wanaoendelea kumtukana rais, litaishia kuhesabu matusi tu na mwisho wake sheria itachukua mkondo wake.