Makonda awaagiza wananchi kutupa taka kwa wenyeviti Serikali za Mitaa

Muktasari:

  • Amesema katika mpango huo anategemea kuona mambo manne yakifanyika ikiwamo suala zima la usafi, utalii.


Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amewataka wananchi wa mkoa huo ambao maeneo yao yamekaa na takataka muda mrefu bila kuzolewa kwenda kuzitupa nyumbani kwa wenyeviti wa Serikali za Mitaa.

Ameyasema hayo leo Machi 17, kwenye hafla ya uzinduzi wa mpango wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam wa kuendeleza utalii wa jiji hilo.

Makonda amesema haiwezekani tunakuja na mpango wa utalii lakini jiji bado linaonekana chafu na kutaka kila kiongozi kuwajibika katika kulisimamia hilo.

“Nawaambieni wananchi kuanzia leo kama mna uhakika mmelipa tozo ya kuzolea taka na taka hizo hazijazolewa kwa muda mrefu, zipelekeni nyumbani kwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mitaa yenu halafu yeye atajua wapi pa kuzipeleka,” amesema Makonda.

Amesema katika mpango huo anategemea kuona mambo manne yakifanyika ikiwamo suala zima la usafi, utalii, stendi za mabasi za kisasa na masoko ya kisasa ambayo yatawawezesha wafanyabiashara kufanya shughuli zao mahali pazuri.

Kwa upande wake Waziri wa Tamisemi, Suleiman Jaffo, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla hiyo, ameupongeza uongozi wa mkoa wa Dar es Salaam kwa kuja na mpango huo na kuahidi kwamba ofisi yake itatoa ushirikano kuona jambo hilo linafanikiwa.