Malori 103 yenye shehena za mahindi yakamatwa

Muktasari:

  • Magari hayo yamekamatwa ikiwa ni siku mbili tangu Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa apige marufuku utoroshaji mahindi na kuagiza kutaifishwa mahindi na malori yatakayokamatwa.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema zaidi ya magari 103 yenye shehena za mahindi yamekamatwa yakiwa katika harakati za kusafirisha mahindi hayo kuyapeleka nchi jirani ya Kenya.

Magari hayo yamekamatwa ikiwa ni siku mbili tangu Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa apige marufuku utoroshaji mahindi na kuagiza kutaifishwa mahindi na malori yatakayokamatwa.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo (Jumatano), Mghwira alisema magari hayo yalikamatiwa eneo la Himo wilayani hapa huku akipiga marufuku usafirishwaji wa nafaka pamoja na sukari kwenda nchi jirani bila ya kuwa na kibali maalumu.

“Baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakisafirisha sukari na nafaka nyakati za usiku huku wakishirikiana na baadhi ya askari polisi ambao si waaminifu, ni vema askari hao wakaacha mara moja kwani ni kinyume cha maadili ya kazi zao,”amesema mkuu huyo wa mkoa.

Amesema mkoa huo una ziada ya chakula tani 62,468 za wanga na tani 4,522 za protini na kwamba wilaya ya Rombo haina uhaba wa chakula kama baadhi ya wafanyabiashara wanavyodai.