Mama Mobeto ataka Hamisa aolewe na huyu

Muktasari:

Shufaa amesema sababu ya kutaka aolewe na mtu wa aina hiyo ni kutokana na wanaume wa kiafrika kutokuwa na mapenzi ya kweli.

Mama wa mwanamitindo, Hamisa Mobeto, Shufaa Rutiginga amesema katika maisha yake alikuwa anamuombea  mtoto wake huyo aolewe na mzungu.

Akizungumza na MCL Digital, Shufaa amesema sababu ya kutaka aolewe na mtu wa aina hiyo ni kutokana na wanaume wa kiafrika kutokuwa na mapenzi ya kweli.

“Unajua mtoto wangu ni mzuri, mrefu ana  shingo  nzuri nataka mwanaume atakayemuoa amuangalie kama malaika, kama malkia kwa kuwa ni mwanamke mwenye misimamo yake na ametulia sio muhuni kama watu wanavyomfikia.

“Wazungu hawana ‘stress’ wanajua namna ya kujali mwanamke, hawanaga mambo ya longolongo linapokuja suala zima la mapenzi tofauti na wanaume wetu wa kiafrika,”amesema.

Kuhusu suala la kuzaa na wanaume tofauti, mama Hamisa amesema hilo kwake halimpi shida na angependa amletee wajukuu wengi zaidi kwa kuwa yeye alijaliwa kumzaa peke yake na kudai kwamba hao ndio ndugu zake.

Ni kutokana na hilo, amesema anatamani amzalie watoto sita, kwa kuwa sasa hivi ana nguvu za kulea wajukuu zake na siku hayupo duniani hao ndio watakuwa ndugu zake na kuweza kumsaidia.

Mpaka sasa Hamisa ana watoto wawili.