Mambosasa asema watu tisa wamefariki kutoka na mvua

Muktasari:

Watu hao wamefariki kutokana na mvua za siku tatu mfululizo ambapo baadhi yao walikutwa wanaelea kwenye mito mbalimbali na kuangukiwa na ukuta

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema watu tisa  wameripotiwa kupoteza  maisha kutokana na mvua zinazoendelea huku watu sita wamejeruhiwa kwa kudondokewa na ukuta na wanaendelea na matibabu.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu, Aprili 16 amesema watu hao wamefariki kutokana na mvua za siku tatu mfululizo ambapo baadhi yao walikutwa wanaelea kwenye mito mbalimbali na kuangukiwa na ukuta.

“Leo nimezunguka kwa helkopta kwa kweli maeneo mengi yameathirika kutokana na mvua zinazoendelea na kusababisha madaraja kuondoka na sehemu nyingine maji kupita juu ya barabara  ikiwemo eneo la Kijichi, Buguruni, Jangwani na Kigamboni," amesema Mambosasa.