Mange Kimambi atajwa michango ya Lissu

Mange Kimambi

Muktasari:

 

  • Mange amesaidia katika  kuhamasisha uchangiaji wa fedha za matibabu ya Lissu

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amewashukuru Watanzania wanaoendelea kumchangia Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu akiwataja wanaoongoza katika kuhamasisha uchangiaji mitandaoni akiwamo Mange Kimambi na Wema Sepetu.

Mbowe amesema mpaka leo Ijumaa jumla ya Sh204 milioni zimepatikana katika michango hiyo pamoja na msaada wa hali ambao wamekuwa wakipewa na Watanzania.

“Tunawashukuru wanaoendelea kuchangisha, tunamshukuru Mange Kimambi kwa kuwahamasisha diaspora kuchangia na katika mitandao akishirikiana na Wema Sepetu na wengine,” alisema Mbowe.

Mange alianzisha kampeni ya kumchangia Lissu katika mtandao wa Gofundme akilenga kupata dola za Marekani  50,000 na mpaka kufikia leo saa 10.41 katika mtandao huo kiasi cha dola za Marekani 23,380 ilikuwa imepatikana ambayo ni wastani wa Sh51.3 milioni.