Maombi kwa Lissu yapigwa 'stop' Sumbawanga

Muktasari:

Chadema mkoani Rukwa walitaka kufanya maombi kwa ajili ya Lissu lakini yakazuiwa

Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema) mkoani Rukwa, leo Jumatano kimeshindwa kufanya maombi maalumu kwaajili ya kumuombea Mbunge Singida Mashariki,  Tundu Lissu aliyejeruhiwa kwa risasi hivi karibuni baada ya polisi mkoani humo kuzuia kwa kueleza kuwa haliruhusu mkusanyiko.

Mwenyekiti wa Chadema mkoa huo,  Sadrick Malila amesema wameskitishwa sana na hatua ya jeshi hilo kwani suala la kumuombea mbunge  huyo kamwe lisingeweza kusababisha uvunjifu wa amani.

Amesema kuwa Chadema mkoa ilikuwa imewaalika viongozi wa dini kutoka makanisa mbalimbali na wachungaji walikuwa tayari wamejiandaa kwaajili ya maombi hayo,  lakini wamelazimika kusitisha baada ya Kamanda wa Polisi, George Kyando kuwaeleza kwamba  wasitishe. 

Mwenyekiti huyo aliwatangazia wanachama wa Chadema na wananchi wengine waliokuwa na nia ya kumuombea Lissu kuwa kila mtu afanye maombi binafsi kwani anaamini Mungu ni mwema na atajibu maombi yao.

Malila alitumia fursa hiyo kuliomba jeshi la polisi kuhakikisha linawasaka watu wanaoitwa kuwa hawafahamiki waliomjeruhi Lissu kwa risasi pamoja na ofisa wa jeshi aliyejuruhiwa kwa kupigwa risasi juzi jijini Dar es Salaam wanasakwa mpaka wapatikane ili kukomesha vitendo hivyo.

"Naliomba sana polisi kama wameshindwa kulinda raia na mali zao, basi waache kulinda mali watalinda wananchi wenyewe wao wawalinde raia tu kwa kuwa inawezekana majukumu yamewazidia wabaki na kitu kimoja na wanachi wawasaidie kitu kingine," alisema.