Marekani yatahadharisha raia wake kuhusu maandamano

Muktasari:

Maandamano hayo ni yale yanayotajwa hasa kwenye mitandao ya kijamii kwamba yatafanyika Aprili 26

Dar es Salaam. Ubalozi wa Marekani nchini umetoa tahadhari kwa wananchi wao wanaoishi Tanzania kuhusu maandamano ya kisiasa yanayotarajiwa kufanyika Aprili 26.

Maandamano hayo yanatarajiwa kufanyika siku ya Muungano huku baadhi ya wanasiasa wakiwa tayari wameshafunguliwa kesi mahakamani kutokana na tuhuma mbalimbali.

Ubalozi umetoa tahadhari kwa raia wake wote kwamba siku ya Aprili 26 wanatakiwa kuwa makini kwa sababu inawezekana kabisa maandamano yakatokea.

Kwenye taarifa hiyo ambayo imetolewa kwa vyombo vya habari imesema kwamba polisi wamejiandaa kukabiliana na maandamano hayo.

“Polisi wanaweza wakatumia mabomu ya machozi na risasi za moto ili kudhibiti maandamano hayo  hivyo ni muhimu kukaa mbali na waandamanaji hao.

Serikali ya Marekani inawatakia kila la kheri raia wa Marekani kwa kuwataka kukaa mbali na makundi ya watu siku hiyo ya Aprili 26 na kufuatilia taarifa kwenye vyombo vya habari ili kujua kinachoendelea.