Maria Nyerere akumbusha mshikamano

Mjane wa Baba wa Taifa, Mama Maria Nyerere

Dar es Salaam. Mjane wa Baba wa Taifa, Mama Maria Nyerere amesema wananchi wanatakiwa kushikamana ili kuleta maendeleo nchini.

Mama Maria alisema hayo nyumbani kwake Mikocheni jana wakati kamati ya ulinzi na usalama ya Wilaya ya Kinondoni ilipokwenda kufanya usafi wa mazingira eneo hilo ikiwa ni sehemu ya kumuenzi muasisi wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Kamati hiyo iliyoongozwa na mwenyekiti wake, Ally Hapi ilifika eneo hilo saa moja asubuhi ikiwa na askari 417 kutoka idara mbalimbali likiwamo Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), Magereza pamoja na Jeshi la Polisi.

Mjane huyo ambaye alikuwa mke wa rais wa kwanza, aliipongeza kamati hiyo kwa kazi waliyoifanya kwa kuunganisha nguvu na kufanya kazi pamoja.

“Suala la kulinda na kutunza mazingira liwe kichwani. Ukibaki kusema mimi, mimi huwezi kufika mbali na ukitaka kurudi kuwa sisi inakuwa ngumu,” alisema.

“Watu wanapokutana kwa ajili ya usafi wanapata nafasi ya kubadilishana mawazo kuhusu masuala yanayogusa maisha yao.”

Pia, alipongeza uongozi wa Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli kwa kuanza kusahihisha makosa yaliyofanywa na baadhi ya watu wasio waaminifu.

“Lazima tukubali makosa na tujisahihishe. Mambo mengine yanauma sana lakini kujikosoa kutafanya tuendelee mbele,” alisema.

Hapi ambaye pia ni mkuu wa wilaya hiyo alisema kupitia kufanya usafi wa makazi hayo ni njia mojawapo ya kumuenzi Baba wa Taifa kwa vitendo.

Hapi alisema Mwalimu Nyerere alipingana na maadui watatu ambao ni ujinga, maradhi na umasikini hivyo usafi ni sehemu ya kuunga mkono vita aliyoianzisha hasa kupinga maradhi yanayotokana na uchafu ya mazingira. Kumbukumbu ya Baba wa Taifa inafanyika nchini kesho.