Matukio manne kutikisa Septemba Mosi

Askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wakiwa katika mazoezi huko Monduli, Arusha. Jeshi hilo litaadhimisha miaka 52 ya kuanzishwa kwake Septemba Mosi kwa kufanya usafi katika mitaa mbalimbali ya nchi.

Muktasari:

Matukio hayo ni kupatwa kwa jua kitendo kitakachotokea kwenye usawa wa anga ya Tanzania katika eneo la Rujewa mkoani Mbeya na lile la Waziri Mkuu kuhamia rasmi Dodoma ikiwa ni kutekeleza ahadi yake aliyoitoa mara baada ya Rais John Magufuli kutangaza azma ya Serikali yake kuhamia huko katika kipindi cha miaka minne na ushee ya utawala wake kilichobaki.

Dar es Salaam. Alhamisi ya Septemba Mosi wiki hii itakuwa siku ya aina yake nchini kutokana na kubeba matukio makubwa manne moja likiwa la kimataifa litakalofanya macho mengi duniani kuelekezwa Tanzania.

Matukio hayo ni kupatwa kwa jua kitendo kitakachotokea kwenye usawa wa anga ya Tanzania katika eneo la Rujewa mkoani Mbeya na lile la Waziri Mkuu kuhamia rasmi Dodoma ikiwa ni kutekeleza ahadi yake aliyoitoa mara baada ya Rais John Magufuli kutangaza azma ya Serikali yake kuhamia huko katika kipindi cha miaka minne na ushee ya utawala wake kilichobaki.

Mengine mawili ni maadhimisho ya miaka 52 ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ambayo yataambatana na kufanya usafi katika mitaa mbalimbali nchini huku kukiwa na tangazo la Chadema la kufanya maandamano na mikutano isiyo na kikomo nchini katika kile chama hicho cha upinzani kilichoeleza kuwa ni operesheni ya Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania (Ukuta) ambayo hata hivyo, imezuiwa na Jeshi la Polisi.

Chadema kimekuja na operesheni hiyo kikidai kwamba hatua kauli ya Rais John Magufuli kuzuia shughuli za kisiasa za majukwaani hadi mwaka 2020 ni ukandamizaji wa haki na demokrasia.

Kauli hiyo ya Chadema iliungwa mkono na vyama vyenye uwakilishi bungeni ambavyo mwishoni mwa wiki iliyopita vilitoa msimamo wa pamoja vikisema kwamba iwapo Rais hapendi kukosolewa, apeleke bungeni muswada wa hati ya dharura wa kufuta vyama vyote vya siasa nchini, kauli iliyotolewa siku moja tangu Jeshi la Polisi kupiga marufuku mikutano ya ndani ya kisiasa kwa madai kuwa ina lengo la kupanga uchochezi.

Baadhi ya wanachama na viongozi wa Chadema wamekamatwa maeneo mbalimbali nchini na baadhi kufikishwa mahakamani kwa madai ya kutoa kauli za uchochezi.

Mvutano huo kati ya polisi na Chadema umewalazimu viongozi mbalimbali wa dini kufanya mikutano kadhaa ya usuluhishi na kuitaka Serikali na Chadema kuifikiria amani ya Tanzania kwa kutafuta njia muafaka za kumaliza tofauti hizo.

Mufti wa Tanzania, Sheikh Mkuu, Abubakar Zubeir alitaka madai ya Chadema yasipuuzwe, bali yasikilizwe na yapatiwe ufumbuzi badala ya kutumia nguvu kuyapuuza huku Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Frederick Shoo akieleza kuwa hali wanayoiona haiwafurahishi hata kidogo.

Juzi, Rais Magufuli alikutana ana kwa ana na aliyekuwa mgombea urais wa Chadema na Ukawa, Edward Lowassa na kupeana mikono, katika maadhimisho ya miaka 50 ya ndoa ya Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa na mkewe Anna.

Kitendo cha mahasimu hao waliochuana vikali katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka jana, kupeana mikono kinazidi kuibua maswali mengi na tafsiri ya tukio la maandamano na mikutano ya hadhara litakalofanywa na Chadema.

 

Maadhimisho JWTZ

Siku hiyo pia JWTZ itaadhimisha miaka 52 ya kuanzishwa kwake kwa kufanya usafi kwenye maeneo mbalimbali huku jeshi hilo likieleza kuwa halitafanya maandamano kwa kuwa Serikali imeyazuia.

Jeshi hilo liliundwa upya Septemba 1964 baada ya kuvunja lile lililorithiwa kutoka ukoloni la Tanganyika Rifles ambalo liliasi Januari 20, 1964.

Msemaji wa JWTZ, Kanali Ngemela Lubinga alisema shughuli ya kufanya usafi pamoja na upandaji miti, itafanyika katika maeneo mbalimbali nchini hadi siku ya kilele cha maadhimisho hayo. Pia, wanajeshi watajitolea damu katika hospitali za jeshi.

Kadhalika, madaktari wa JWTZ watatoa huduma za tiba bure kama upimaji wa virusi vya Ukimwi, kisukari na shinikizo la damu na kushiriki michezo mbalimbali baina yake, taasisi mbalimbali.

 

Kupatwa kwa jua

Tukio la kupatwa kwa jua litakalodumu kwa takriban saa mbili, ni la aina yake kwa kuwa hutokea kwa nadra na baadhi ya dini zinawataka waumini wake wakati wa kipindi hicho kuwa kwenye swala maalumu.

Watu wanaoishi katika ukanda wenye upana wa kilomita 100 unaokatisha Kusini mwa Tanzania, kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC) kuelekea Katavi, Mbeya, Ruvuma hadi Masasi na kuingia Msumbiji, siku hiyo wataona jua kama duara jembamba mithili ya pete, kwa vile asilimia 98 ya jua katika maeneo yao litakuwa limejificha nyuma ya mwezi.

Wataalamu wameeleza kuwa wananchi wanaweza kushuhudia kupatwa kwa jua kwa usalama kwa kutumia miwani maalumu ya mwanga wa jua.

Wapo ambao wataitumia siku hiyo kujifunza sayansi ili kuelewa kwa nini kinatokea kile watakachokiona, tukio linaloweza kutumiwa na shule na taasisi za elimu kuendeleza sayansi na kuvutia wanafunzi.

Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) imesema tukio hilo litafungua milango kwa sekta ya utalii katika Nyanda za Juu Kusini kwa kuwa watalii na watafiti kutoka ndani na nje ya nchi watembelea maeneo hayo kushuhudia tukio hilo la kipekee duniani.

Kaimu Mkurugenzi Mwendeshaji wa TTB, Philip Chitaunga alisema Bodi hiyo imeandaa safari ya watu 50 itakayowajumuisha wanahabari na watu maarufu nchini kwa ajili ya kushuhudia tukio hilo la kihistoria.

“Sekta ya utalii ndiyo inayoongoza kuiingizia nchi pato la kigeni… hivyo tukio hili tunaliona kama ni fursa itakayoutangaza utalii wa Kusini. Kusini kwa sasa miundombinu ni mizuri, kuna uwanja mkubwa wa ndege, barabara zinapitika, hivyo Tanzania itafahamika zaidi,” alisema Chitaunga.

 

Waziri Mkuu kuhamia Dodoma

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kuhamia Dodoma ni miongoni mwa matukio yatakayotikisa Septemba Mosi, ikiwa ni utekelezaji wa kauli ya Rais Magufuli ya kutaka Serikali kuhamia mjini humo baada ya jambo hilo kushindikana tangu kutangazwa kwake miaka ya 70.

Julai 24 mwaka huu, Majaliwa alieleza dhamira yake ya kuhamia Dodoma ifikapo Septemba ili kuonyesha kuwa Serikali imedhamiria kutekeleza ahadi inazotoa kwa wananchi.

Alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa Dodoma na kuwashukuru kwa ushiriki wao kwenye maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa zilizofanyika kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Mashujaa, mjini humo.

Akizungumzia tukio hilo, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Christina Mndeme amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi siku hiyo kumpokea Waziri Mkuu.

“Maandalizi yanaendelea vizuri na ninawaomba wakazi wa Dodoma kujitokeza kwa wingi kumpokea Waziri Mkuu kwa sababu hili ni tukio la kihistoria.”